ONYESHO la mavazi ‘Fashion for Peace’ limezindua vazi maalumu kwa ajili ya kuhamasisha amani kuelekea uchaguzi mkuu wa Oktoba 25.
Onyesho hilo lililofanyika mwishoni mwa wiki katika Ukumbi wa King Solomon, Dar es Salaam liliwajumuisha wabunifu, Mustafa Hassanali, Martin Kadinda na Kiki Zimba.
Onyesho hilo lilifunguliwa na mwanamitindo wa Tanzania anayefanya kazi zake barani Ulaya, Tausi Likokola, aliyevalia vazi la mbunifu Kiki Zimba kwa kuzingatia umuhimu wa amani.
Martin Kadinda alibuni nguo zilizovaliwa na wanamitindo wa kiume, nguo hizo nyingi zikiwa na rangi ya njano na nakshi za kijani zililenga kubeba rangi tatu kuu zilizopo katika bendera ya taifa.
Naye Mustafa Hassanali, nguo zake zilipambwa na rangi ya njano na dhahabu pamoja na vito vilivyotengenezwa na ‘Phoebe Jewellery’.