23.3 C
Dar es Salaam
Friday, April 26, 2024

Contact us: [email protected]

Samatta atwaa tuzo Ubelgiji

Na BADI MCHOMOLO, DAR ES SALAAM

NAHODHA wa timu ya taifa ya Tanzania (Taifa Stars) anayecheza soka la kulipwa katika klabu ya K.R.C Genk ya Ubelgiji, Mbwana Samatta, ametwaa tuzo ya mchezaji bora wa Afrika 2019 kwa wachezaji wanaokipiga katika Ligi ya nchini Ubelgiji.

Tuzo hizo zilitolewa usiku wa kuamkia jana, ambapo tuzo aliyochukua Samatta hutolewa kwa mchezaji bora anayetoka Afrika na kucheza soka la kulipwa nchini Ubelgiji.

Tuzo hiyo inajulikana kwa jina maarufu la Ebony Shoe Award. Samatta anakuwa mchezaji wa tatu wa K.R.C Genk kuwahi kutwaa tuzo hiyo katika historia yake.

Mchezaji wa kwanza wa K.R.C Genk kuwahi kutwaa tuzo hiyo ni Souleymane Oulare, raia wa Guinea, ambaye alishinda tuzo hiyo 1999, baada ya kucheza soka kwa kipindi cha miaka mitatu tangu 1996.

Mchezaji mwingine ni Moumouni Dagano, raia wa Burkina Faso aliyeshinda tuzo hiyo 2002, baada ya kuitumikia timu hiyo tangu mwaka 2001 hadi 2003.

Pamoja na hayo, Samatta hadi sasa anaongoza kwa ufungaji wa mabao ya Ligi Kuu Ubelgiji, akiwa amefunga jumla ya mabao 23. Kuna uwezekano mkubwa wa mchezaji huyo kutwaa tuzo ya mfungaji bora msimu huu.

Mwaka 2015, mchezaji huyo aliandika historia kwa soka la Tanzania baada ya kutwaa tuzo ya mchezaji bora wa mwaka kwa wachezaji wanaocheza ndani, wakati huo alikuwa anakipiga katika klabu ya TP Mazembe, kabla ya kujiunga na K.R.C Genk.

Samatta kwa sasa ni miongoni mwa wachezaji wenye mchango mkubwa katika klabu ya K.R.C Genk katika mbio za kuwania taji la Ligi Kuu Ubelgiji msimu huu, wakihitaji pointi 4 kuwa mabingwa na wamesalia na michezo mitatu ili kumaliza Ligi.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles