23.7 C
Dar es Salaam
Friday, April 19, 2024

Contact us: [email protected]

Mahakama yabariki Serikali kutaifisha mali za DECI

NA KULWA MZEE

DAR ES SALAAM

MAHAKAMA  Kuu Kanda ya Dar es Salaam, imebariki  Serikali  kutaifisha mali na Sh bilioni 14.2 za iliyokuwa Kampuni ya Development Entrepreneurship for Community Initiative (DECI) baada ya kujiridhisha kwamba zilitokana na mchezo haramu wa upatu.

Uamuzi huo  ulitolewa jana na Jaji Stephen Magoiga  aliyekuwa akisikiliza shauri hilo na kusema wajibu maombi wameshindwa kuwasilisha vielelezo vyakupinga maombi ya Mkurugenzi wa Mashtaka Nchini (DPP) Biswalo Mganga, kutaka mali hizo zitaifishwe na kuwa mali ya Serikali.

DPP aliwasilisha mahakamani hapo maombi namba 42 ya mwaka huu dhidi ya waliokuwa viongozi wa DECI Jackson Sifael Mtares, Dominick Kigendi, Timotheo Saiguran Ole Loitg’nye na Samwel Sifael Mtares.

Jaji Magoiga alisema kutokana na kutokuwepo kwa ushahidi huo, mahakama imeyakubali maombi ya DPP kama yalivyo na kutoa maelekezo saba kama ifuatavyo.

Mali zote zilizoorodheshwa katika kiapo cha DPP zitaifishwe na kuwa mali ya serikali, pili Mameneja wa matawi ya Benki  zilizotajwa kuhifadhi fedha za Deci wazipeleke fedha hizo serikalini mara baada ya kupelekewa amri ya mahakama.

Tatu malizote ambazo ni nyumba na viwanja vilivyotajwa katika shauri hilo zisajiliwe kwa  jina la Msajili wa Hazina kutoka jina la Deci,nne ,mali au viwanja ambavyo havijapimwa vipimwe na kusajiliwa kwa jina Msajili wa Hazina.

Tano, DPP apeleke maombi mahakamani kuomba madalali wa mahakama kwa ajili ya kuwaondoa watu wanaoishi katika nyumba zilizotajwa katika shauri hilo,sita magari yote yabadilishwe umiliki na kuwa mali ya serikali na saba Kamishna wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) ameelekezwa kubadilisha umilikiwa  wa gari hizo na kuwa mali ya serikali.

Awali akisoma uamuzi huo, Jaji Magoiga alisema amezingatia hoja za pende zote mbili katika hauri hilo ikiwa ni pamoja na kuzingatia sheria inayoongoza namna ya kutaifisha mali zilizotokana kwa njia ya uhalifu ambapo kifungu namba 9 hadi 15 kinajitoshereza katika utekelezaji wake.

“Viapo  vinahitaji ushahidi, unaeleza ukweli na ikibidi unaleta ushahidi, pasipo kuwepo ushahidi maana yake wameshindwa kupinga hoja za DPP, nimepitia kiapo chenu na kugundua kwamba kinamapungufu,” alisema Jaji Magoiga na kuongeza kwamba alitegemea wajibu maombi wangeonyesha chanzo kingine cha mapato.

Awali DPP Mganga aliwasilisha maombi hayo mahakamani hapo, akiiomba itoe amri ya kutaifishwa kwa mali za kampuni hiyo yakiwemo magari 11, nyumba na viwanja vinane na fedha ziwe nali ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Mali hizo ni nyumba namba UKMMD/1237 iliyoko Mwembe Madafu, Ukonga, Dar es Salaam, kiwanja namba 651, kitalu ‘M’ kilichopo Forest area, Mbeya, nyumba iliyoko kiwanja namba 7, kitalu ‘P’  ikiwa na hati namba  033004/23 kilichopo mtaa wa Rufiji, Manispaa ya Mwanza.

Mali nyingine ni ardhi iliyoko katika kiwanja namba 2/283/2 kitalu “E” Mabibo, Kinondoni, Dar es Salaam, kipande cha ardhi ambacho hakijapimwa kilichopo kijiji cha Manyinga, Turiani, Mvomero, Morogoro, kiwanja namba 467 kilichopo kitalu “H” kikiwa na hati ya usajili namba 48170 kilichopo eneo la Tegeta, Dar es Salaam, nyumba iliyoko kiwanja namba MM/19/P kilichopo Manzese karibu na barabara ya Morogoro, Dar es Salaam na nyumba iliyoko katika kiwanja namba KND/MXS/MNM/Z ikiwa na leseni ya makazi namba KND 008337 Kinondoni, Dar es Salaam.

Magari  ni Toyota Premio lenye namba  T 132 AWJ, Toyota Land Cruiser namba T 480 AUP,   Toyota Rav 4 namba T 274 ATQ, Toyota Mark II namba T 676 AYP, Subaru Legacy namba T 682 AUT, Toyota Ipsum namba T 850 AXY, Toyota Ipsum  T455 ADM, Toyota Mark II T 186 AYX, Mitsubishi Pajero  T 852 AAV, Toyota Lande Cruiser T 789 AUX, Nissan Terrano namba T 899 AYU.

Aliomba amri ya kutaifishwa kwa fedha zilizoko benki katika akaunti namba 22601601056 iliyoko National Microfinance Bank (NMB), tawi la Msasani  ikiwa n ash. 12,503,068,647.89.

Fedha nyingine taslim ni zilizoko katika akaunti namba 000120100000194/1 iliyoko Dar es Salaam Community Bank (DCB), tawi la Uhuru ikiwa na sh. 1,457,700,462.49 na fedha taslim zilizoko katika akaunti namba 021140019558 iliyoko Kenya Commercial Bank (KCB), tawi la Samora, Dar es Salaam, ikiwa na Sh 57,933,304

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles