23.4 C
Dar es Salaam
Saturday, April 27, 2024

Contact us: [email protected]

Majambazi yatikisa Zanzibar

mtz1Na Mwadishi Wetu, Zanzibar
MAJAMBAZI yametikisa viunga vya Mtaa wa Darajani kisiwani Zanzibar na kusimamisha shughuli za biashara wakati polisi walipowakimbiza na kuamua kutumia risasi za moto.
Tukio hilo lilitokea jana saa nane mchana na kusababisha watu wawili kujeruhiwa na watatu kupoteza fahamu kutokana na vishindo vya risasi na mabomu wakati majambazi hayo yalipotaka kutoroka.
Taarifa zaidi zinasema gari ya majambazi hayo iliwagonga wanawake wawili baada ya kuingia kwa kasi katika eneo la wafanyabiashara wa Darajani maarufu kwa jina la Jua Kali.
Baadhi ya mashuhuda wa tukio hilo walisema majambazi hayo yalikuwa na gari aina ya Toyota Noah yalikimbizana na polisi na walipofika katika kituo cha zamani cha daladala walipotea njia kwa kutaka kupita kulia kabla ya gari yao haijakwama katika ukuta wa Shule ya Msingi Darajani.
Mkazi wa Michenzani, Said Musa Ali, alisema wakati wakishangaa gari hiyo kuingia kwa kasi, ghafla wanawake wawili waligongwa na kusukumwa pembeni huku wengine wakipiga kelele baada ya milio ya risasi kutokea.
Alisema ndani ya gari hiyo kulikuwa na dereva na abiria watatu na waliteremka wakiwa na silaha wakataka kukimbia.
Naye, Halima Mohamed, alisema akiwa amejificha chini ya meza aliona moja kati ya majambazi hayo akipigwa risasi kichwani na kudondoka chini huku mwezake akizungukwa na wananchi waliokuwa na hasira.
Alisema dereva wa gari hiyo alitoka upande wa kushoto na kufanikiwa kuruka ukuta wa shule hiyo wakati tayari wananchi wakimkimbiza.
“Kama si mlipuko wa risasi, wananchi walimkamata dereva yule mguu wakati anaruka ukuta lakini kwa bahati mbaya wakati wanamshika kulitokea kishindo cha risasi wakamwacha baada ya kukumbwa na hofu,” alisema Omar Suleiman.
Baadhi ya wafanyabiashara wadogo katika eneo hilo walitupa vifaa vya kufanyia biashara zao baada ya kutokea milio ya risasi.
Akizungumzia tukio hilo, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Mjini Magharibi, Mkadam Khamis Mkadam, alisema majambazi hayo yalikuwa yamegawanyika makundi mawili huku wengine yakifanikiwa kukimbilia katika eneo la Fumba lililopo nje ya mji.
Alisema operesheni ya kuwasaka majambazi hayo na dereva aliyekimbia inaendelea kufanyika kwa ustadi mkubwa.
“Tukio hilo lilitokea saa nane mchana na kusababisha biashara kusimama kwa muda katika eneo hilo huku watu wakikimbia ovyo baada ya askari wa kikosi cha kupambana na ujambazi kuanza kurusha risasi wakati wakitafuta njia ya kuwakamta majambazi hayo yakiwa salama.
“Wafanyabiashara wa Soko la Darajani walioshuhudia tukio hilo walisema kwamba ulikuwa kama mchezo wa kuigiza wakati askari hao wakikimbizana na majambazi hayo na kusababisha njia kuu ya Darajani kufungwa kwa muda baada ya majambazi kupotea njia na kuingia katika barabara isiyopitisha magari.
“Hali ilikuwa mbaya kila mtu alishindwa kuamini baada ya kuanza kusikia milio ya risasi watu wakikimbia ovyo, jambo la kushukuru wananchi walifanya ujasiri mkubwa kwa kushirikiana na polisi hadi kuwakamata wakiwa na silaha zao,” alisema Mkadam.
Katika hatua nyingine, Mganga wa zamu wa Hospitali ya Rufaa ya Mnazi Mmoja Zanzibar, Dk. Marijani Msafiri, alisema watu watano walifikishwa hospitalini hapo wakiwemo majeruhi wawili wanaoendelea na matibabu.
Alisema kati ya hao, wengine walikuwa wakisumbuliwa na tatizo la kutojitambua kutokana na mshituko na kukumbwa na hofu lakini waliendelea kutibiwa.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles