23.4 C
Dar es Salaam
Saturday, April 27, 2024

Contact us: [email protected]

KOMBE LA DUNIA LINAWEZA KUWA NDOTO KWA DEMBELE

Na BADI MCHOMOLO


WACHEZAJI wengi kipindi hiki cha michuano ya Ligi Kuu wamekuwa wakionesha kiwango cha hali ya juu ili kuisaidia klabu yake pamoja na kujitafutia nafasi ya kuitwa kwenye kikosi cha timu ya Taifa kwa mataifa ambayo yamefuzu kushiriki michuano hiyo.

Kushiriki Kombe la dunia ni kitu muhimu sana kwa wachezaji ambao wanataka kuandika historia ya soka duniani kwa kuwa ni michuano ambayo inafanyika mara moja ndani ya miaka minne tofauti na Ligi zingine.

Kipindi hiki kwenye Ligi wanaonekana wachezaji makinda kutoka klabu mbalimbali wakiuwasha moto wao ili kuweza kuwashawishi makocha, huku ikidaiwa kwamba makocha wengi wanapenda kutumia damu changa kwenye michuano hiyo.

Ousmane Dembele, kinda ambaye amefanya makubwa kwenye michuano ya Ligi Kuu nchini Ujerumani msimu wa 2016 hadi 2017 akiwa na kikosi cha Borussia Dortmund na kuwashawishi vinara wa Ligi Kuu nchini Hispania kuweka historia ya usajili wake hadi kutua Nou Camp.

Kinda huyo mwenye umri wa miaka 20, alitamba sana akiwa na klabu hiyo ya Ujerumani, lakini baada ya kujiunga na Barcelona kwa uhamisho wa Euro milioni 105, mwaka jana hadi sasa bado amekuwa kwenye wakati mgumu kutokana na kusumbuliwa na majeruhi.

Hadi sasa tangu ajiunge amefanikiwa kucheza jumla ya michezo minne ya Ligi Kuu, mara ya kwanza alipata majeruhi ya nyama za paja na kumfanya akae nje ya uwanja kwa miezi mitatu kutokana na kufanyiwa upasuaji, mwanzoni mwa mwezi huu alipata nafasi ya kurudi uwanjani lakini alicheza michezo miwili yote akicheza dakika chache na hatimaye akapata majeruhi mengine.

Majeruhi haya ya sasa yanamfanya mchezaji huyo kuwa nje ya uwanja kwa mwenzi mmoja, hivyo mwezi wa pili mwishoni anaweza kuonekana tena viwanjani, hali hiyo ya kusumbuliwa na majeruhi ya mara kwa mara yanaweza kumfanya kuwa katika wakati mgumu wa kuitwa kwenye kikosi cha timu ya Taifa ya Ufaransa.

Atakuwa na kazi kubwa ya kurudi uwanjani kwa kasi kama ilivyokuwa wakati anakipiga Dortmund, kasi hiyo anatakiwa kuifanya kwa kipindi cha miezi mitatu kabla ya kumalizika kwa Ligi mwezi wa tano na mwezi unaofuata kuingia kwenye Kombe la dunia.

Dembele hana nafasi kubwa sana katika timu ya Taifa, lakini wengi walitarajia kumuona akifanya vizuri msimu huu nchini Hispania akiwa na kikosi cha Barcelona ili aweze kupata nafasi kubwa ndani ya Ufaransa. Mwaka juzi ilikuwa mara yake ya kwanza kuitwa timu ya Taifa, hivyo hadi sasa amefanikiwa kucheza jumla ya michezo saba tangu aitwe.

Kikubwa amuombe Mungu aweze kupoma mapema na hasipate majeruhi tena kwa kipindi kilichobaki hadi kumalizika kwa Kombe la dunia, hata hivyo akirudi uwanjani ndani ya Barcelona anatakiwa kuonesha uwezo wa hali ya juu ili kuwashawishi wafaransa wampe nafasi.

Timu ya Taifa ya Ufaransa ni moja ya timu ambayo inatabiriwa kufanya makubwa kwenye Kombe la dunia msimu huu kutokana na ubora wa wachezaji wao kama vile Paul Pogba, Antoine Griezmann, Kylian Mbappe, N’golo Kante, Anthony Martial, Thomas Lemar, Blaise Matuidi, Alexandre Lacazette na wengine wengi wanaofanya vizuri kwenye klabu zao.

Mwaka 2016, timu hiyo walikuwa wenyeji wa michuano ya Kombe la Euro, walifanikiwa kufika fainali na hatimaye timu ya Taifa ya Ureno ilifanikiwa kutwaa taji hilo.

Umri wa Dembele ni mdogo, hivyo bado ana nafasi kubwa ya kushiriki michuano ya Kombe la dunia mara nyingi, ila kuanza kucheza michuano hiyo ukiwa na umri mdogo kuna raha yake.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles