24.1 C
Dar es Salaam
Friday, April 26, 2024

Contact us: [email protected]

Yanga yakamilisha hesabu

NA MOHAMED KASSARA

TAYARI wamekamilisha hesabu, hivyo ndivyo ilivyo ndani ya kikosi cha Yanga baada ya kukamilisha usajili wao na kuanza kambi kujiandaa na msimu mpya wa Ligi Kuu Tanzania Bara na Ligi Mabingwa Afrika.

Mapema wiki hii, kikosi cha Yanga kilitua mkoani Morogoro kuanza kambi, lakini bila Kocha Mkuu wao, Mwinyi Zahera aliyekuwa mapumzikoni nchini Ufaransa, baada ya majukumu ya timu ya taifa ya DR Congo, iliyotolewa katika michuano ya Kombe la Mataifa ya Afrika (Afcon2019), nchini Misri.

Yanga, pia imejichimbia huko ili kusuka kikosi imara tayari kurudisha heshima yao katika michuano ya kimataifa baada ya kupata tiketi ya kushiriki Ligi ya Mabingwa Afrika msimu ujao.

Katika kuhakikisha haeindi kusindikiza katika michuano hiyo, Yanga imefanya usajili wa maana, ikinasa wachezaji wa ndani pamoja na wa kimataifa ili kukiongezea makali kikosi chao.

Wachezaji wa kimataifa waliotua Yanga ni Sadney Urikhob raia wa Namibia, Lamine Moro (Ghana), Juma Balinya (Uganda), Issa Bigirimana (Burundi) na Patrick Sibomana (Rwanda), Moustapha Selemani (Burundi), Maybin Kalengo (Zambia) na Farouk Shikalo kutoka Kenya.

Wazawa ni Ally Mtoni ‘Sonso’ (Lipuli), Ally Ally (KMC), Mapinduzi Balama (Alliance FC), Muharami Issa (Malindi), Abdulaziz Makame (Mafunzo) na Metacha Mnata (Mbao).

Baadhi ya wachezaji hao tayari wapo kambini Morogoro wakijufia vikali chini ya Kocha msaidizi, Noel Mwandila aliyeachiwa jukumu la kukiongoza kikosi hicho kabla ya kurejea kwa Zahera wikiendi hii.

Akizungumza na waandishi wa habari jana, Ofisa Habari wa Yanga, Dismas Ten, alisema sehemu kubwa ya wachezaji wao tayari wamesharipoti kambini, huku akieleza kuwa Urikhob anatarajiwa kuoneka mazoezini kuanzia leo.

Alisema kuanza mazoezi kwa mshambuliaji huyo, kutakamilisha hesabu zao, kwani wachezaji wao wote tayari watakuwa wameanza maandalizi ya kuelekea msimu mpya wa Ligi Kuu Bara.

“Kambi yetu inaendelea vizuri kule Morogoro, wachezaji wote wamefika, isipokuwa kwa wale waliokuwa timu ya taifa ambao nao hadi kufikia Jumapili, watakuwa wameungana na wenzao.

“Urikhob anatarajia kuingia nchini leo (jana), akitokeoa kwa Namibia ambapo alikuwa na matatizo ya kifamilia yaliyomfanya kuchelewa kujiunga na wenzake, lakini tumewasiliana naye na ametuambia tayari amemaliza matatizo hayo na atawasili kabla kesho (leo) kujiunga na wenzake kambini,” alisema.

Ten alisema tayari timu hiyo imekamilisha usajili wa wachezaji watakaowatumia katika michuano ya kimataifa na majina 26 yameshatumwa Shirikisho la Soka Afrika (Caf).

Hata hivyo, Ten alishindwa kuweka wazi kama jina la mlinda mlango wao mpya, Shikalo ni miongoni mwa yaliyotua Caf.

Yanga ilimsajili Shikalo akiwa na mkataba wa miezi sita na timu yake ya Bandari, lakini pande hizo mbili zilikubaliana amalize kwanza kukitumikia kikosi chake katika michuano ya Klabu Bingwa Afrika Mashariki na Kati (Kombe la Kagame) kabla ya kujiunga na wababe hao wa Jangwani.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles