25.2 C
Dar es Salaam
Friday, April 26, 2024

Contact us: [email protected]

“Wazazi watakaoshindwa kupeleka watoto shule kudeki vyoo”

Na Ramadhan Hassan,Dodoma

MKUU wa Mkoa wa Dodoma, Anthony Mtaka ameagiza wazazi na walezi watakaoshindwa kuwapaleka watoto wao shule kufikia Jumatatu ya wiki ijayo kukamatwa na kupewa kazi ya kufanya usafi katika vyoo vya shule pamoja na katika miradi ya Serikali ambayo inaendelea kujengwa mkoani hapa.

Amesema Jumatatu ya wiki ijayo( Januari 31, 2022) atafanya msako wa nyumba kwa nyumba kujua ambao watakuwa wamekaidi agizo lake hilo na kudai kwamba Magereza huwa haijai.

Agizo hilo amelitoa leo Januari 28,2022 wakati alipokuwa akizungumza na wazazi, walimu na wanafunzi wa shule ya sekondari Zuzu ambayo katika matokeo ya kidato cha nne mwaka jana shule hiyo imeshika nafasi ya 51 katika shule 52 zilizofanya mtihani wa kidato cha nne.

Mkuu huyo wa Mkoa amewataka watendaji wa mitaa ya Mazengo, Pinda, Sokoine, Soweto na Chididimo katika Kata ya Zuzu Jijini hapa kuhakikisha wanafunzi wote waliochaguliwa kujiunga na kidato cha kwanza wanafika shuleni haraka ili kuanza masomo mara moja.

Amesema kwa kutumia migambo wanatakiwa kuwakamata wale wote ambao watakuwa wamekaidi agizo hilo ikiwa ni pamoja na kuwapa jukumu la kufanya usafi katika vyoo vya shule pamoja na katika miradi ya Serikali.

“Mzazi ambaye mwanae atakuwa hajaripoti shuleni akamatwe akasafishe vyoo huku watoto wakiwa wanaona ikiwezekana wawe vibarua katika miradi inayoendelea kujengwa na Serikali akiwa kapeleka mtoto wake Private simu ipigwe shuleni waulizwe,”amesema.

Amesema katika hilo hatanii na atalisimamia kwa nguvu zake zote huku akidai kwamba wale wote watakaofanya hivyo atahakikisha wanakimbia nyumba zao.

“Sitaki kusikia mtoto anabaki nyumbani anataka aje shule,kwangu mtaelewa kwanguvu na hapa ninamanisha sina utani katika hili hatuwezi kujenga nitahakikisha mpaka mnakimbia nyumba zenu sitaki utani katika hili,”amesema Mtaka.

Aidha, RC Mtaka amesema atafanya msako wa nyumba kwa nyumba kuwatafuta wale wote ambao watakuwa wamekaidi agizo hilo huku akitaka kila mzazi kubeba jukumu lake.

Amewataka wazazi kuwasaidia wanafunzi waweze kutimiza ndoto zao za kusoma na kuacha kulalamika kwamba wanatembea umbali mrefu.

“Kila mzazi abebe hasira za kuhakikisha mwanae anasoma na kufaulu agenda ya elimu iwe kipaumbele kwa kila mmoja sitaki kusikia habari ya maneno maneno wanafunzi wanatakiwa kusoma,”amesema.

Awali, Mwenyekiti wa Bodi ya shule, Dismas Chilala amesema wanakabiliwa na changamoto ya uelewa wa wazazi na wanafunzi kuhusu umuhimu wa elimu kwani wengi wamekuwa hawamalizi shule kutokana na sababu mbalimbali.

“Hapa changamoto Mheshimiwa Mkuu wa Mkoa ni mtazamo wa elimu ni nini katika jamii na manufaa yake ni yapi,hapa wengi wanaoanza kusoma hawamalizi,”amesema

Kwa upande wake, Diwani Kata ya Zuzu,Awadh  Abdallah amesema changamoto kubwa ambayo wanakutana nayo ni wanafunzi waliochanguliwa kujiunga na kidato cha kwanza kuchukuliwa na kwenda kufanya kazi za ndani pamoja na wengine kutokuripoti shuleni.

Amesema kunahitajika jitihada kuhakikisha wanafunzi wanaoonza kidato cha kwanza kuwasaidia mpaka wamalize kidato cha nne kwani wengi wamekuwa hawamalizi.

Amesema  changamoto ya wanafunzi kutembea umbali mrefu wa kilomita 6 kutoka Chididimo hadi Zuzu aliitatua kwa kutoa nyumba ili wanafunzi waweze kukaa na kutakiwa watoe Sh 15,000 lakini wengi walikataa.

Naye, mmoja wa wazazi, Ernest Chisota amesema changamoto kubwa wanayokutama nayo ni ukosefu wa maabara pamoja na baadhi ya walimu kutoingia darasani.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles