25.2 C
Dar es Salaam
Friday, April 26, 2024

Contact us: [email protected]

WAVAA NGUO FUPI, MILEGEZO SASA KUKIONA

Na OMARY MLEKWA-SIHA


KATIBU Mwenezi wa CCM Wilaya ya Siha mkoani Kilimanjaro, Cosmas Uwisso, ameishauri halmashauri ya wilaya hiyo kutunga sheria ya kuwapiga faini wale wote wanaovaa nguo fupi zenye kuonyesha maumbile.

Amesema sheria hiyo pia iwabane wanaume wote wanaovaa suruali za kubana (vimodo) na milegezo hususani watumishi wa umma ambao wamekuwa chanzo kikuu cha mmomonyoko wa maadili kwenye jamii.

Hayo aliyasema mwishoni mwa wiki alipokuwa akizungumza na wanafunzi wa shule za sekondari, walimu, wazazi na viongozi wa dini katika maadhimisho ya Wiki ya Jumuiya ya Wazazi wa chama hicho yaliyofanyika katika viwanja vya CCM wilayani hapa na kusema lazima halmashauri itunge sheria ya kuwabana wale wote wanaochangia mmomonyoko wa maadili ikiwemo watumishi wa umma.

“Watumishi wengi wamechangia sana kuendeleza kumomonyoka kwa maadili kutokana na kushindwa kuvaa mavazi yenye staha, hali ambayo watoto wetu wanaona  ni sahihi na kuiga.

“Ni vema itungwe sheria ndogo na halmashauri ambayo itaruhusu kupigwa faini kwa yeyote atakayekutwa amevaa nguo zisizokuwa na maadili na sheri hii pia itasaidia kuongeza mapato ya ndani,” alisema.

Kwa upande wake, Sheikh wa Mtaa wa Sanya, Mohamed Hamza, alisema  wazazi wamekuwa chanzo kikuu cha  mmomonyoko wa madili kutokana na kushindwa kukemea pindi wanapowaona watoto wao wakifanya mambo yasiyoendana na tamaduni zao.

“Wazazi sasa hivi hawawezi kukemea vitendo viovu vinavyofanywa na watoto wao kutokana na baadhi yao kuwa sehemu ya mmomonyoko wa maadili na wengine kukosa muda wa kuzungumza na watoto wao,” alisema.

Naye Mchungaji Deamen Moshi wa Kanisa la Kiinjili la Kilutheri Tanzania (KKKT), Usharika wa Sanya Juu, alisema kuporomoka kwa maadili kunasabishwa na kutokutii mafundisho ya Mungu, wazazi na hata

walimu wanaowafundisha.

“Vijana wanatakiwa kujikita katika elimu wawapo shuleni na kujifunza kusema hapana kwa mambo ambayo si  sahihi  kwenye jamii na vijana walio mitaani wajitume kufanya kazi badala ya kuzurura  mitaani na kukaa vijiweni,” alisema.

Kwa upande wake, Katibu wa Wilaya wa  Jumuiya  hiyo, Masumbuko Mahinya, alisema vijana wengi wamekuwa na tabia za kuiga tamaduni za watu wa  nchi za nje pindi wanapoona wageni wanakuja nchini wakiwa wamevaa nguo tofauti.

“Vijana wetu wanaiga kutoka kwa wageni pamoja na kuangalia sinema na kuona kuwa ni sahihi kuvaa mavazi yasiyoendana na tamaduni zetu, jambo hili lazima kila mmoja wetu alikemee ili  vijana wetu wasizidi kupotea,” alisema.

 

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles