23.4 C
Dar es Salaam
Saturday, April 27, 2024

Contact us: [email protected]

Watu 4,000 hufa maji kila mwaka Ziwa Victoria

SHEILA KATIKULA- MWANZA

SERIKALI imesema zaidi ya watu 4,000 hufa maji kila mwaka Ziwa Victoria kutokana na sababu mbalimbali, ikiwamo hali halisi ya vyombo vya usafiri, uwezo wa mabaharia, ubebaji mizigo, hali ya hewa, pamoja na ziwa hilo kutofanyiwa vipimo kujua maeneo yenye miamba na kina kirefu tangu ilipofanyika mara ya mwisho kabla ya uhuru mwaka 1961.

Hayo yalisemwa na Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Wakala wa Meli Tanzania (Tasac), Emmanuel Ndomba, wakati akizungumza  katika mkutano wa wadau wa vyombo vya majini jijini Mwanza.

Ndomba alisema ili kupunguza idadi ya wanaokufa maji, Tasac imeamua kuweka vituo vya uokozi na mawasiliano.

“Tunaposema ajali ni nyingi Ziwa Victoria, hatusemi kwa Watanzania pekee, tunasema na nchi zingine kama Kenya na Uganda, namba zinazoonyeshwa kutoka kwenye data walizonazo Lake Victoria Basin, zipo kwenye watu 4,000 kwa mwaka.

“Kuna watu wengine wanakufa wanazika tu hivyo hivyo, haiwi ‘reported’, kuna vile vijiji ambavyo vipo kandokando mtu anakufa kwa sababu ya maji, watu wanaamua kuzika tu hivyo hivyo wala hawahitaji kuripoti, lakini idadi ipo kwenye 4,000.

“Tupo kwenye mikoa 11 Tanzania, mikoa yote ya maji, kwa sababu kazi zetu tunazozifanya zinakwenda kwenye vituo vya  forodha vyote, pia kwenye vituo vyote vya maji, yaani baharini na kwenye maziwa.

“Lake Victoria tupo sana kwa sababu ni ziwa ambalo lina watu wengi sana wanaolizunguka, na maisha yao yote yanategemea kinachopatikana katika hili ziwa na ndilo linaloongoza kwa ajali,” alisema Ndomba.

Alisema yanayofanyika katika Ziwa Victoria yanahusu nchi tatu za Kenya, Uganda na Tanzania, hivyo mara kwa mara hukutana pamoja ili kupanga mikakati.

Naye Meneja wa TRA Mkoa wa Mwanza, Joseph Mtandika amemshukuru Rais Dk. John Magufuli kwa kuanzisha Tasac hali itakayochangia upatikanaji wa mapato halisi.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles