23.4 C
Dar es Salaam
Saturday, April 27, 2024

Contact us: [email protected]

WANAFUNZI 900,000 KUFANYA MTIHANI LA SABA LEO

Na NORA DAMIAN – DAR ES SALAAM

WANAFUNZI 917,072 wa darasa la saba, leo wanatarajia kuanza mtihani wa kumaliza elimu ya msingi (PSLE), utakaomalizika kesho.

Idadi hiyo ni ongezeko la watahiniwa 121,311, ikilinganishwa na 795,761, waliohitimu elimu hiyo mwaka 2016.

Katibu Mtendaji wa Baraza la Mitihani Tanzania (NECTA), Dk. Charles Msonde, akizungumza na waandishi wa habari jana, alisema mtihani huo utafanyika kwa siku mbili na utahusisha masomo matano ya Kiswahili, Kiingereza, Hisabati, Sayansi na Maarifa ya Jamii.

Alisema watahiniwa 882,249 watafanya mtihani kwa Kiswahili na wengine 34,823 kwa Kiingereza, lugha ambazo wamekuwa wakizitumia kujifunzia.

Watahiniwa 94 wakiwamo wavulana 58 na wasichana 36 ni vipofu huku wengine 1,138 wakiwa na uoni hafifu ambao uhitaji maandishi makubwa.

“Maandalizi yote yamekamilika, karatasi za mitihani, fomu maalumu za kujibia na nyaraka zote muhimu zinazohusu mtihani huo zimesambazwa katika halmashauri na manispaa zote nchini,” alisema Dk. Msonde.

Alitoa wito kwa kamati za mitihani za mikoa na halmashauri kuhakikisha kuwa mazingira ya vituo vya mitihani yapo salama, tulivu na kuzuia mianya yote inayoweza kusababisha udanganyifu.

“Wasimamizi, watahiniwa, walimu, wamiliki wa shule na wananchi wote tunawaasa kutojihusisha na vitendo vya udanganyifu, na watahiniwa watakaobainika watafutiwa matokeo yao.

“Tunaamini kuwa walimu wamewaandaa wanafunzi vizuri, hivyo tunatarajia watafanya mtihani huo kwa kuzingatia kanuni za mtihani ili matokeo yaonyeshe uwezo wao halisi kulingana na maarifa na ujuzi waliopata,” alisema.

Baraza hilo pia liliwataka wamiliki wa shule kutambua kuwa shule zao ni vituo maalumu vya mtihani, hivyo hawatakiwi kuingilia majukumu ya wasimamizi wa mtihani.

Katibu huyo alisema hatosita kukifuta kituo chochote cha mtihani endapo atajiridhisha kuwa uwepo wake unahatarisha usalama wa mitihani ya taifa.

Baraza hilo lilitoa wito kwa jamii kutoa ushirikiano kuhakikisha mtihani huo unafanyika kwa amani na utulivu na kuepuka kuingia kwenya maeneo ya shule katika kipindi chote cha mtihani.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles