23.4 C
Dar es Salaam
Saturday, April 27, 2024

Contact us: [email protected]

UHURU KENYATTA AANZA KUMTOA JASHO RAILA

NAIROBI, KENYA

KATIKA uchaguzi wowote wa kisiasa kura za maoni ni jambo muhimu sana. Mara nyingi kura hizo ni utafuti unaoendeshwa na taasisi mbalimbali ili kupata maoni ya wananchi juu ya wagombea mbalimbali kwenye uchaguzi mkuu.

Hali hiyo ndiyo imetokea nchini Kenya, ambapo kura za maoni zimewashtua wachambuzi wa masuala ya siasa nchini humo na kudai kuwa huenda ikawa kura halisi hapo Agosti 8 mwaka huu.

Ripoti ya utafiti ya Infotrak iliyotolewa Ijumaa wiki hii imebainisha kuwa Uhuru Kenyatta anayo nafasi kubwa ya kumshinda mpinzani wake Raila Odinga, kutoka muungano wa vyama vya upinzani, NASA. Ripoti hiyo imesema endapo uchaguzi ungefanyika leo Uhuru Kenyatta angeshinda kwa asilimia 48 dhidi ya asilimia 43 za Raila Odinga.

Ripoti hiyo imesema chama cha Jubilee kimekuwa maarufu zaidi  nchini Kenya huku muungano wa NASA ukishika nafasi ya pili kwa umaarufu.

Kura za maoni zinaonyesha kuwa asilimia 50 ya Wakenya wanasema nchi yao inakwenda kombo hivyo ushindi wa Uhuru Kenyatta utaongeza matatizo zaidi kama atamshinda Raila Odinga.

Hata hivyo Infotrack wamesema kuwa kuna maeneo mbalimbali ambayo yanaweza kuwaibua na kura nyingi wagombea hao.

Mathalani wanasema Uhuru Kenyatta amekuwa maarufu zaidi kuliko Raila Odinga, ambapo anaungwa mkono zaidi katika maeneo ya kati ya Kenya.

Aidha, Infotrack wanasema mgombea ambaye angeshika nafasi ya tatu Abduba Dida kwa kujizolea asilimia 0.5 ya kura zote. Wengine Ekuru Aukot, Cyrus Jirongo  na Joe Nyaga wanmgegawana asilimia 0.1.

Kura hizo za maoni zilikusanywa na kati ya Juni 24 na 27, imebainishwa kuwa uchaguzi huo unaweza kuingia kwenye raundi ya pili na kuwakutanisha tena Uhuru na Raila.

Sababu kubwa inayotolewa ni kwamba kila mmoja angetamba kuibuka na ushindi, lakini watalazimika kufikisha asilimia 50 ya kura zote.

Mshindi wa Uchaguzi Mkuu wa mwaka huu ataamuliwa kwa kura za jumla. Taasisi ya Infotrak imeeleza kutumia sampuli za wtau 2000 ili kupata matokeo yao.

Idadi hiyo inawakilisha watu milioni 19.6 ambao wameandikishwa na Tume ya Uchaguzi (IEBC) kupiga kura mwaka huu.

KURA ZA KENYATTA

Takwimu za ripoti Infotrak zinaonyesha kuwa Uhuru Kenyatta anaungwa mkono katika maeneo ya ukanda wa Kati kwa asilimia 90, Kaskazini Mashariki asilimia 75, Mashariki asilimia 58, na Bonde la Ufa asilimia 56.

Hata hivyo Uhuru Kenyatta angepata kura chache mno katika maeneo haya Nyanza asilimia 14,  Magharibi asilimia 28, Pwani asilimia 29, na Nairobi asilimia 41.

KURA ZA ODINGA

Raila Odinga anaungwa  katika maeneo ya Nyanza asilimia 83, Pwani asilimia 61, Magharibi asilimia 53 na Nairobi asilimia 51.

Naye Raila Odinga angepata kura chache kwenye maeneo haya; Kati asilimia 5, Kaskazini Mashariki asilimia 20, Bonde la Ufa asilimia 4  na Mashariki asilimia 37.

Aidha, utafiti huo unaonyesha kuwa chama cha Jubilee ni maarufu zaidi nchini Kenya ambapo kinafahamika miongoni mwa wananchi kwa asilimia 47. Hilo ni tofauti na muungano wa upinzani NASA ambao unafahamika miongoni mwa wananchi wa Kenya kwa asilimia 43

Chama cha Jubilee ni maarufu zaidi katika maeneo ya Kati asilimia 88 na maeneo ya Nyanza asilimia 14, wakati muungano wa upinzani NASA unafahamika  maeneo ya Nyanza kwa asilimia 83 ambapo ni pungufu kwa asilimia 5. Pia NASA kinafahamika maeneo ya Kati-Kenya kwa asilimia 5 tu wakati Jubilee ni asilimia 88.

Ni dhahiri utafiti huo umeonyesha tofauti ya vyama hivyo kwa kila eneo nchini humo.

WANASIASA WATIWA KUFULI

Wakati takwimu za uchaguzi mkuu zikitolewa na Infotrak, upande mwingine wanasiasa wametiwa kufuli  na mamlaka ya Mawasiliano nchini humo baada ya kupiga marufuku vyama vya siasa kutuma ujumbe mfupi kutumia lugha za makabila.

Hatua hii imechukuliwa kupambana na lugha za uchochezi kipindi hiki cha kampeni kuelekea Uchaguzi Mkuu.

Utaratibu huo uliotolewa na Tume hiyo ya Mawasiliano pamoja na Tume ya uwiano na utengamano, inavitaka vyama vya siasa nchini humo kutumia lugha ya Kiswahili na Kiingereza pekee katika mawasiliano yake.

Aidha, lengo la utaratibu huu mpya ni kuwazuia wanasiasa kuepuka kutumia lugha ya uchochezi kutumia mitandao ya kijamii kama Facebook, Whats App, Twitter na YouTube.

Kampuni za simu nchini humo sasa zitahitaji kupitia ujumbe uliotumwa na kuuwasilisha kwa mamlaka hayo ili kupitiwa kubaini ikiwa kuna matamshi ya uchochezi yanaendelea kutolewa. Hatua hii imetajwa ni kukomesha siasa za kikabila amabzo zimekuwa zikitawala chaguzi za Kenya kila mara.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles