25.2 C
Dar es Salaam
Friday, April 26, 2024

Contact us: [email protected]

Ubingwa Ligi Kuu bado upo rehani

simba yangaNA ADAM MKWEPU, DAR ES SALAAM

WAKATI mbio za kuwania ubingwa wa Ligi Kuu Tanzania Bara msimu huu zimeshika kasi, hakuna dalili yoyote inayoonyesha kama mchezo kati ya Yanga dhidi ya Azam utakaochezwa Jumamosi Uwanja wa Taifa Dar es Salaam utatoa bingwa wa ligi hiyo.

Yanga itaingia kwenye mchezo huo ikiwa inaongoza ligi kwa kuwa na pointi 46 sawa na Azam, ambayo inashikilia nafasi ya pili kwa tofauti ya mabao ya kufunga na kufungwa huku Simba ikiwa nafasi ya tatu baada ya kujikusanyia pointi 45 katika mechi 20 ilizocheza.

Yanga imefunga mabao 44 na kufungwa 9, huku Azam ikiwa imeziona nyavu za wapinzani wake mara 34 na kufungwa 11 kutokana na mechi 19 walizocheza ikiwa ni pointi moja nyuma ya Simba, ambayo imefunga mabao 35 na kufungwa 13.

Pambano la Yanga dhidi ya Azam litachezwa huku timu zikiwa zimebakiwa na michezo 10 kila moja, wakati Simba imebakiwa na 9 ili kupatikana bingwa wa Ligi Kuu msimu huu.

Michezo hiyo itakuwa na jumla ya pointi 30 ili timu iweze kuwa kwenye nafasi nzuri ya kujihakikishia ubingwa inatakiwa kunyakua zaidi ya pointi 15 hadi 18.

Pointi hizo zinatokana na kuwapo kwa michezo 10, ambapo mitano kati ya hiyo inawezekana kutoa taswira halisi ya bingwa msimu huu.

Yanga itacheza mechi 6 ugenini, huku 4 ikicheza katika uwanja wake wa nyumbani, Azam itacheza michezo mitano ikiwa kwenye dimba lake la Azam Complex na mingine mitano ikiwa ugenini, wakati Simba itacheza mechi 3 ugenini na mingine 6 ikiwa uwanja wake wa nyumbani.

Moja ya mechi zinazoonekana kuwa ngumu kwa timu zilizopo kwenye nafasi tatu za juu ni ule utakaochezwa Aprili 2 kati ya Yanga na Kagera Sugar katika Uwanja wa Taifa, siku chache baadaye Azam itakutana na Toto Africans kwenye Uwanja wa CCM Kirumba.

Presha itapanda zaidi Aprili 16 wakati Simba ikiikaribisha Azam kwenye Uwanja Taifa, Dar es Salaam, ambapo siku moja baadaye Yanga nao wataikaribisha Mgambo Shooting kwenye uwanja huo.

Aidha, mchezo wa Machi 13 wa Simba dhidi ya Prisons utakuwa miongoni mwa michezo migumu ya mwishoni mwa msimu, ambayo inaweza kuwa na matokeo yasiyotarajiwa.

Bingwa wa Ligi Kuu msimu huu anaweza kufikisha pointi 64 ambazo ni nyingi, ukilinganishwa na msimu uliopita wakati bingwa alikuwa na jumla ya pointi 55.

Kutokana na hesabu hiyo, huenda bingwa wa msimu huu akapatikana baada ya michezo itakayochezwa kuanzia Aprili, ambapo timu nyingi zitakuwa zimefikia michezo kuanzia 25 na kubakiza mitano.

Hatua hiyo inafanya nafasi ya ubingwa kuwa wazi kwa timu zote tatu zilizopo kileleni mwa msimamo wa ligi hiyo.

Kwa kuwa michezo iliyochezwa na timu za Ligi Kuu hadi sasa ni 20 kati ya 30, Yanga na Azam zitakuwa zikikamilisha hesabu hiyo huku zikiwa na viporo vya mchezo mmoja mkononi.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles