27.9 C
Dar es Salaam
Thursday, March 28, 2024

Contact us: [email protected]

Twiga Stars kuivaa Zimbabwe leo

pg32     2NA SUZANA MAKORONGO, (RCT)

TIMU ya Taifa ya soka ya wanawake ‘Twiga Stars’, inatarajia kujitupa katika Uwanja wa Azam Complex leo kuvaana na Zimbabwe katika mchezo wa kuwania tiketi ya kufuzu kucheza fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika kwa wanawake, zitakazofanyika Cameroon Novemba mwaka huu.

Twiga inaingia uwanjani tayari ikiwa imepewa motisha na Serikali, kukabidhiwa kitita cha shilingi milioni 15 kama ikishinda mchezo wa kwanza, ambapo kila mchezaji atapewa shilingi 300,000, timu hiyo itapewa tena kiasi hicho kwenye mchezo wa marudiano nchini Zimbabwe ikishinda.

Akizungumza Dar es Salaam jana, kocha wa timu hiyo, Nasra Juma alisema atatumia mfumo wa 4-4-2, akieleza mfumo huo unatosha kabisa kuiua timu ya Zimbabwe katika mchezo wao wa leo.

“Kwa jinsi alivyowasoma wapinzani wetu, naamini kwa kutumia mfumo huu nitabakisha ushindi nyumbani na kujiandaa kwenda kuwamaliza wakiwa nchini kwao.

“Naomba Watanzania wajitokeze kwa wingi kushuhudia timu yao inavyotoka kifua mbele katika mchezo huo,” alisema.

Alisema hana shaka na wachezaji wake kwani amewapa mazoezi ya kutosha tangu Februari 7 kujiandaa na mchezo, hali iliyowafanya kujipima nguvu na timu ya wanaume ya Veteran ambapo walionyesha kiwango kizuri.

Wakati huo huo, nahodha wa timu hiyo, Sophia Mwasikili, alisema watahakikisha wanayafanyia kazi mafunzo yote waliyopewa na mwalimu, ili kushinda katika mchezo huo na kujiwekea nafasi nzuri ya kufuzu kushiriki fainali hizo.

“Tunawaahidi Watanzania kuwaletea matokeo mazuri, ukizingatia Mheshimiwa Naibu Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Anastazia Wambura atakuwepo, hivyo hatutaweza kuwaangusha tutahakikisha tunaipeperusha bendera ya Tanzania vema,” alisema.

Timu hizo zinatarajiwa kurudiana kati ya Machi 18 au 20, nchini Zimbabwe.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles