30.5 C
Dar es Salaam
Sunday, May 12, 2024

Contact us: [email protected]

Tucta yataka likizo ya uzazi iongezwe kwa wanaojifungua watoto njiti

Na Nora Damian, Mtanzania Digital

Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi Tanzania (TUCTA) limeiomba Serikali kuangalia upya likizo ya uzazi kwa wanaojifungua watoto njiti ili wapate muda zaidi wa kuwaangalia watoto hao.

Kulingana na Sheria ya Ajira na Mahusiano Kazini ya mwaka 2004 na kanuni zake za mwaka 2017, mwanamke aliyejifungua ana haki ya kupewa likizo ya uzazi ya siku 84 akijifungua mtoto mmoja na siku 100 akijifungua watoto mapacha.

Aidha kifungu cha 33 (10) kinampa haki ya kupata ruhusa ya saa mbili kwa siku kwa ajili ya kumnyonyesha mtoto.

Mkurugenzi wa Shirika la Kazi Duniani anayeshughulikia nchi za Afrika, Fantan Kayirangwa (Kushoto), akimsikiliza Katibu Mkuu wa Shirikisho la Vyama vya Wafanyakazi Tanzania, Hery Mkunda, alipotembelea ofisi za shirikisho hilo Dar es Salaam. Katikati ni Mkurugenzi wa ILO Afrika Mashariki, Caroline Mugalla.

Tucta imewasilisha changamoto hiyo leo Februari 6,2024 kwa Mkurugenzi wa Shirika la Kazi Duniani anayeshughulikia nchi za Afrika, Fantan Kayirangwa, ambaye alitembelea shirikisho hilo.

Katibu Mkuu wa Tucta, Hery Mkunda, amesema wanawake wengi wanaojifungua watoto njiti wamekuwa wakikaa muda mrefu hospitali kutokana na changamoto hiyo hali inayosababisha kuwa na muda mchache wa kupumzika.

“Tunaomba suala hili liangaliwe upya, muda ambao mama anakaa hospitali na mtoto njiti isiwe miongoni mwa siku 84,” amesema Mkunda.

Shirikisho hilo pia limetaja changamoto nyingine kuwa ni ajira kwa watoto hasa katika migodi na mashambani na ushirikishwaji wa wanawake katika maeneo ya kazi.

Tucta imeliomba ILO kuwajengea uwezo viongozi wa vyama vya wafanyakazi ili waweze kujadiliana na kushughulikia masuala ya wafanyakazi vizuri.

Katibu Mkuu huyo amesema pia changamoto mbalimbali walizowasilisha wakati wa Mei Mosi mwaka 2023 zimefanyiwa kazi ikiwemo kuongezwa kwa vitendea kazi na watendaji hasa katika Wakala wa Usalama Mahala pa Kazi (OSHA).

“Tunamshukuru Rais Samia tangu aingie madarakani mambo mengi ya wafanyakazi anayatafutia suluhisho. Kabla ya Mei Mosi ya 2023 asilimia 90 ya yale tuliyowasilisha kwake mwaka 2022 alikuwa ameyafanyia kazi…ya mwaka 2023 yamefanyiwa kazi kwa kiwango kikubwa,” amesema Mkunda.

Naye Mkurugenzi wa ILO Afrika, Kayirangwa amesema wataendelea kushirikiana na Tanzania kuboresha masuala mbalimbali ya wafanyakazi.

“Nimefurahishwa na hatua ambazo Tanzania imechukua katika kutekeleza maelekezo ya ILO, tutaendelea kuwajengea uwezo katika nyanja ya utumishi, majadiliano na masuala yote yanayohusu wafanyakazi,” amesema Kayirangwa.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
587,000SubscribersSubscribe

Latest Articles