23.4 C
Dar es Salaam
Saturday, April 27, 2024

Contact us: [email protected]

Trump, Putin kukutana Ufaransa

 MOSCOW, URUSI

RAIS Vladimir Putin anatarajiwa kukutana na Rais wa Marekani, Donald Trump. Kukutana kwa wawili hao kunakuja baada ya Trump kutishia kuwa nchi yake itajiondoa kutoka mkataba wa kudhibiti silaha za nyuklia kati ya Urusi na Marekani (INF).

Kufuatia kitisho hicho cha Marekani, Putin amesema anataka kukutana na Trump kwa mazungumzo jijini Paris, Ufaransa. Tangazo la kushtukiza la Trump kujiondoa katika mkataba huo limezua hisia tofauti kwa viongozi wa mataifa ya Ulaya.

Kwa mujibu wa Mshauri wa Usalama wa Taifa wa Marekani, John Bolton, Putin alisema yuko tayari kukutana na Trump hivi karibuni. Wawili hao wanatarajiwa kuonana Novemba 11, watakapokuwa katika sherehe za kuadhimisha miaka 100 ya kumalizika kwa vita ya kwanza ya dunia.

Bolton aliyekuwa ziarani Urusi alizungumzia mustakabali wa mkataba huo na Waziri wa Mambo ya Nje wa Urusi, Sergey Lavrov pamoja na Mkuu wa Baraza la Usalama la Urusi, Nikolai Patrushev. Baada ya kukutana na Bolton, Patrushev alisema Urusi iko tayari kufanya kazi na Marekani ili kuuokoa mkataba huo.

Mkataba huo uliotiwa saini mwaka 1987 unapiga marufuku makombora ya nyuklia kurushwa kwa zaidi ya umbali wa kilomita 5,500. Lakini Marekani inadai Urusi imekiuka hilo kwa kombora lililorushwa mapema mwaka huu.

Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Kujihami ya Magharibi (NATO), Jens Stoltenberg alisema washirika wote wa Ulaya wanakubali kuwa mkataba huo ni muhimu. “Washirika wote wanakubali kuwa mkataba huu ni muhimu ndio maana tuna wasiwasi juu ya tabia ya Urusi. Kwa hiyo tatizo ni tabia hii, ambayo tumeiona kwa miaka mingi.

“Hii haiwezi kuendelea maana hatuwezi kuwa na mkataba kati ya pande mbili wenye kuheshimiwa tu na upande mmoja,” alisema Stoltenberg.

Waziri wa Mambo ya Nje wa Ujerumani, Heiko Maas alisema mkataba huo ni nguzo muhimu kwa usalama wa Ulaya, lakini Waziri wa Ulinzi wa Uingereza, Gavin Williamson alisema wao wapo pamoja na Marekani kutokana na Urusi kuyadhihaki makubaliano hayo.

Rais wa Poland, Andrzej Duda alisema tangazo la Trump la kujiondoa katika mkataba huo linaeleweka kufuatia shughuli zinazofanywa na Urusi.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles