25.1 C
Dar es Salaam
Thursday, May 2, 2024

Contact us: [email protected]

TANGA BEACH RESORT YAJIPANGA KWA KIWANGO CHA KIMATAIFA

Na mwandishi wetu


TANGA ni moja kati ya miji ya mwambao yenye historia kongwe na yenye kuvutia.

Asili ya jina la Tanga inaaminika kutokana na neno “tanga” – kitambaa kikubwa kinachofungwa kwenye mlingoti wa jahazi.

Pia jina la Tanga kwa kabila la Kibondei ambalo ni wenyeji wa mkoa huo, lina maana ya shamba, wao hulitamka “n’tanga”.

Tanga inasifika kwa kuwa na vivutio vya kipekee vya utalii.

Baadhi ya vivutio hivyo ni mapango ya Amboni, mji mkongwe wa Pangani, Hifadhi ya Saadani, Milima ya Usambara, misitu ya asili ya Amani na vinginevyo.

Pamoja na utalii huo wa asili, sasa kuna mradi wa bomba la kusafirishia mafuta ghafi kutoka Hoima nchini Uganda hadi mkoani humo.

Mbali na mradi huo kuwa kichocheo kipya cha uchumi wa Tanga na Tanzania kwa ujumla, pia  kukamilika kwake kutakua fursa nyingine ya utalii katika mkoa huo.

Kutokana na hali hiyo, watu mbalimbali wa Mkoa wa Tanga na mingine jirani, wanaendelea kujipanga kutumia fursa ya mradi huo wa bomba utakaogarimu Dola za Marekani bilioni 3.5 (Sh trilioni 8).

Miongoni mwa wafanyabiashara waliojipanga kutumia fursa hiyo ni wale wa sekta za utoaji huduma, ikiwamo malazi.

Mojawapo ya watoa huduma hao ni Tanga Beach Resort, hoteli pekee yenye hadhi ya nyota tano katika mkoa huo, ambayo ina hadhi ya kupokea hata rais wa nchi.

Meneja Mkuu wa Tanga Beach Resort, Joseph Ngonyo, ameliambia MTANZANIA kuwa ujenzi wa bomba la mafuta ni neema kubwa kwa wakazi wa mkoa huo.

“Ujenzi wa bomba hili ni fursa kubwa kwa mkoa wetu wa Tanga. Tukiwa watoa huduma katika sekta ya hoteli, tunauona mradi huu kama ni fursa nzuri, tumejipanga kutoa huduma za hoteli kwa kiwango cha kimataifa.

“Kwa vyovyote watu watakaohusika na ujenzi watahitaji chakula, vinywaji na malazi na sisi tupo kwa ajili ya kuwahudumia,” anasema.

Ngonyo anasema ili kuhakikisha wanatumia fursa ya bomba hilo kikamilifu, tayari wameshaanza mpango wa upanuzi wa jengo jipya litakalokuwa na vyumba 72 kukabiliana na ongezeko la wageni.

“Baada ya kukamilika kwa vyumba hivyo 72, hoteli yetu itakuwa na jumla ya vyumba 118 na chumba kimoja chenye hadhi ya kufikiwa na rais (Presidential suit),” anaeleza.

Meneja huyo anafafanua kuwa kwa sasa hoteli hiyo imeajiri watu 98 kupitia ajira za moja kwa moja, huku wengine 32 wakiwa na ajira zisizo za moja kwa moja.

Anasema upanuzi huo ukikamilika ajira zaidi zitaongezeka kwa kuwa watahitajika wafanyakazi wa kuhudumu sehemu mbalimbali ndani ya hoteli hiyo.

“Jamii ambazo zinatuzunguka, pia zitafaidika kupitia bidhaa ambazo hoteli yetu itanunua kutoka kwao kama vile mbogamboga, matunda, nyama, samaki na nyingine,” aliongeza.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles