28.2 C
Dar es Salaam
Wednesday, May 8, 2024

Contact us: [email protected]

Tamisemi, Wizara vya Elimu zawapiga msasa Wanahabari kuhusu mradi wa shule bora

Na Gustafu Haule, Pwani

SERIKALI kupitia Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (TAMISEMI) kwa kushirikiana na Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia imewapiga msasa Waandishi wa Habari wa Mkoa wa Pwani kuhusu umuhimu wa mradi wa Shule Bora ulioanza kutekelezwa nchini mwaka 2021.

Mradi wa Shule Bora nchini unatekelezwa katika mikoa tisa kwa ufadhili wa Serikali ya Uingereza kupitia mfuko wa UKaid ambapo gharama za mradi zitakuwa na bajeti ya Paundi za kiingereza milioni 89 sawa Sh bilioni 271.

 Aidha, mafunzo hayo yaliyofanyika Mjini Kibaha jana yaliwakutanisha Waandishi wa habari kutoka vyombo mbalimbali,maafisa habari,walimu,wawakilishi kutoka Wizara ya elimu na waendeshaji wa mafunzo kutoka Tamisemi na waratibu  wa mradi huo.

Akifungua warsha hiyo Katibu Tawala wa Mkoa wa Pwani Zuwena Omary,amesema kuwa Serikali imekuja na mradi huo kwa lengo la kuimarisha elimu ya awali na msingi kwa watoto wa Kitanzania.

Zuwena, amesema kuwa mambo makubwa yanayolengwa katika mradi wa Shule bora ni kuhusu kujifunza,kufundisha,Jumuishi pamoja na kujenga mfumo ambapo kwa pamoja itasaidia kuinua kiwango cha elimu nchini hususani kwa watoto wa Shule ya awali na msingi.

Amesema kuwa,kutokana na umuhimu wa mradi huo Serikali imeona ni vyema kuwashirikisha waandishi wa habari ili wawe sehemu ya mradi huo na kufanyakazi kwa pamoja ili kutimiza malengo yaliyowekwa na Serikali.

“Serikali ya awamu ya Sita chini Mheshimiwa Rais mama Samia Suluhu Hassan inatambua umuhimu wa kazi inayofanywa na Waandishi wa habari ndio maana imetoa kipaumbele kikubwa katika mradi huu wa Shule bora na Mkoa utaendelea kushirikiana na wanahabari ili kutangaza zaidi mradi wa Shule Bora,” amesema Zuwena

Aidha, Zuwena ametumia nafasi hiyo kuziomba Halmashauri za Mkoa wa Pwani kuhakikisha zinasimamia kikamilifu mradi huo ili uweze kuleta mafanikio makubwa hapa nchini hususani katika kuimarisha elimu katika ngazi ya chini mpaka kitaifa.

Ameishukuru Serikali ya Uingereza kupitia mfuko wake wa UKaid kwa kushirikiana na Serikali ya Tanzania katika kufikia makubaliano ya kutekeleza mradi huo ambao utakwenda kuleta mabadiliko chanya katika masuala ya elimu.

Kwa upande wake afisa mahusiano wa mradi huo, Raymond Kanyambo, amesema kuwa Shule bora ni programu ya Serikali  inayolenga kuinua kiwango cha elimu ya ngazi ya awali na msingi katika Mikoa tisa nchini ukiwemo Mkoa wa Pwani, Simiyu, Tanga, Mara, Dodoma, Katavi, Singida, Rukwa na Kigoma.

Kanyambo amesema kuwa mradi huo ulianza mwaka 2021 na uzinduzi wake ulifanyika Mjini Kibaha katika Shule ya Msingi mkoani na utadumu kwa muda wa miaka Sita lakini ukifanyika vizuri utakuwa endelevu kwa miaka mingine mitatu.

“Shule bora itachangia kuinua ubora wa elimu jumuishi na mazingira salama ya kujifunzia kwa Wavulana na Wanawake na hii Mikoa ilichaguliwa kutokana na changamoto mbalimbali ambazo zinazuia watoto kusoma,” amesema Kanyambo

Nae AfisaElimu Mkoa wa Pwani, Sara Mlaki, amesema kuwa pamoja na mambo mengine lakini lengo la warsha hiyo ni kupitia utekelezaji wa mradi wa Shule bora uliofanyika kwa kipindi cha mwaka mmoja.

Hatahivyo,Mlaki amesema kuwa mafanikio ya mradi huo katika kipindi hicho ni makubwa kwakuwa hali ya utoro, mimba, ndoa na changamoto nyingine zinazowakatisha masomo wanafunzi hususani wakike zimepungua. 

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
587,000SubscribersSubscribe

Latest Articles