31.2 C
Dar es Salaam
Thursday, March 28, 2024

Contact us: [email protected]

FCC yawapa mbinu wafanyabiashara kupata mitaji, teknolojia mpya

Na Norah Damian, Mtanzania Digital

Tume ya Ushindani (FCC) imesema inatoa vibali vinavyowawezesha wafanyabiashara na wawekezaji kuungana ili kupata mitaji na teknolojia mpya.

Akizungumza Desemba 9,2022 Mkurugenzi Mkuu wa FCC, William Erio, amesema wamekuwa wakipitisha maombi ya watu wanaotaka kuungana kibiashara ili kuwawezesha kupata mtaji na teknolojia mpya.

Mkurugenzi Mkuu wa Tume ya Ushindani (FCC), William Erio, akisalimiana na Ofisa Mtendaji Mkuu wa Kampuni ya Sisalana inayozalisha bidhaa za mkonge, Elizabeth Kalambo, wakati alipotembelea mabanda mbalimbali kwenye Maonesho ya Saba ya Bidhaa za Viwanda vya Tanzania.

Erio alikuwa akizungumza kwenye Maonesho ya Saba ya Bidhaa za Viwanda vya Tanzania yaliyofanyika Uwanja wa Mwalimu Julius Nyerere maarufu Sabasaba,

“Watu wanafikiri kwamba kupata mtaji ni lazima uende kukopa benki, na kilio kikubwa cha wafanyabiashara wanasema wanapenda kukopa lakini riba kubwa, njia nyingine ya kupata mtaji kwa urahisi unaweza kuungana na kampuni nyingine iwe ya ndani au ya nje.

“Wakienda katika Kituo cha Uwekezaji Tanzania watakuta orodha ya watu ambao wanasubiri kuja kuwekeza au wana maombi ya kuwekeza hapa nchini, anayekuja si lazima aje na uwekezaji mpya, anaweza akakuunga na wewe mkapanua wigo, mnakuja FCC sisi tunatoa kibali cha kuungana kwahiyo tatizo la mtaji na teknolojia tunakuwa tayari tumelitatua,” amesema Erio.

Amesema pia FCC imekuwa ikishiriki kwenye maonesho hayo na mengine ili kutoa elimu kwa umma uweze kukitambua chombo hicho na shughuli wanazozifanya za kulinda ushindani katika shughuli za kibiashara na kumlinda mlaji.

“Tunashiriki katika maonesho haya kuhakikisha majukumu tuliyonayo kisheria yanatekelezwa kwa ufanisi, tunahakikisha kwamba mlaji na mtumiaji wa bidhaa analindwa na kulinda uwepo wa bidhaa bandia katika soko la nchi yetu,” amesema.

Aidha amewataka wazalishaji kufanya kazi kwa karibu na tume hiyo ili kuhakikisha bidhaa bandia haziingii sokoni na kuwasisitiza kuzalisha bidhaa ambazo hazitaigwa na wengine.  

Katika maonesho tume hiyo ilitoa elimu kwa umma jinsi ya kutambua bidhaa bandia na kuwataka Watanzania kuchukua hatua kujiepusha nazo kwa sababu zina athari kwa afya, zinahatarisha usalama wa mali na maisha na zinaongeza umaskini kwa kulazimu kuzinunua mara kwa mara kutokana na kuharibika haraka.

Maonesho hayo yaliyoanza Desemba 3,2022 na kuhitimishwa Desemba 9,2022 yalikuwa na washiriki 502 na yaliongozwa na kaulimbiu isemayo ‘Nunua bidhaa za Tanzania jenga Tanzania’.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
585,000SubscribersSubscribe

Latest Articles