23.6 C
Dar es Salaam
Saturday, April 27, 2024

Contact us: [email protected]

Simba SC yamtuliza Mo, yaiua Mbao 2-1

NA MWANDISHI WETU -MWANZA

TIMU ya Simba imefanikiwa kuvuna pointi ugenini baada ya kuichapa Mbao FC mabao 2-1 katika mchezo wa Ligi Kuu Tanzania Bara uliochezwa jana kwenye Uwanja wa CCM Kirumba, Mwanza.

Ushindi huo unaweza kumtuliza mwekezaji wao Mohammed Dewji ambaye alitishia kujiuzulu nafasi ya mwenyekiti wa bodi mara baada ya Simba kupoteza fainali ya Kombe la Mapinduzi dhidi ya Mtibwa Sugar.

Mabao ya Simba yalifungwa na Hassan Dilunga dakika ya 41 na Jonas Mkude dakika 46, huku bao la kufutia machozi la Mbao likiwekwa wavuni na Wazir Junior dakika 52.

Ushindi huo inaifanya kikosi hicho cha Wekundu wa Msimbazi kuendelea kujikita kileleni mwa msimamo wa ligi hiyo ikifikisha pointi 38 baada ya kucheza michezo 15, ikishinda 12, sare miwili na kupoteza mmoja.

Kichapo hicho kinaiacha Mbao katika nafasi ya 14 ikiwa na pointi 18 ilizovuna kupitia michezo 17, ikishinda minne, sare sita na kupoteza saba.

Licha ya uwanja kujaa maji kutokana na mvua kubwa iliyonyesha, Simba ilitawala mchezo kwa sehemu kubwa na kufanya mashambulizi mengi kwenye lango la wapinzani.

Simba iliuanza mchezo huo kwa kasi, ambapo dakika ya kwanza tu Ibrahim Ajib alipoteza nafasi ya wazi kuindikia Simba bao baada ya kupokea pasi ya John Bocco, lakini mpira wa kichwa alioupiga ulitua mikononi mwa mlinda mlango wa Mbao, Abdallah Makangana.

Dakika ya tano, Makangana alisimama na kupangua mchomo hatari wa Shomari Kapombe aliyepiga kutoka mbali.

Dakika ya 25, Clatous Chama alipoteza nafasi  nyingine ya kuifungia Simba baada ya kupokea  pasi ya Sharaf Shiboub, lakni mkwaju wake ulishindwa kulenga lango.

Dakika ya 41, Dilunga aliindikia Simba bao la kuongoza kwa shuti kali la mguu kushoto akiwa mbali lililokwenda moja kwa kimiani na kumuacha Makangana akiwa hana la kufanya.

Bao hilo linadumu kwa dakika 45 za kipindi cha kwanza kwani hadi timu zinakwenda mapumziko Simba wapo mbele kwa 1-0.

Kipindi cha pili kilianza kwa kasi na  Simba kuendelea kuutawala mchezo  dakika ya 46, Mkude aliifungia Simba bao la  pili akimalizia  mpira wa kona uliopigwa na  Ajibu.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles