23.6 C
Dar es Salaam
Saturday, April 27, 2024

Contact us: [email protected]

Simba itaendelea kuinyanyasa Biashara United leo?

NA WINFRIDA MTOI-DAR ES SALAAM

TIMU ya Simba inatarajia kushuka dimbani leo kuvaana na Biashara United, katika mchezo wa Ligi Kuu Tanzania Bara, utakaofanyika kwenye Uwanja wa Uhuru, Dar es Salaam.

Wekundu wa Msimbazi hao, wanashuka dimbani wakiwa na hamu ya kupata pointi tatu, baada ya kushindwa kuzichukua kwa Mtibwa Sugar katika mechi yao iliyopita.

Katika mchezo huo uliochezwa wiki iliyopita, Simba iliambulia alama moja, ikitoka sare ya bao 1-1 na Mtibwa, Uwanja wa Jamhuri, Morogoro.

Kabla ya kuikabili Mtibwa, Simba ilizindua kampeni zake za msimu huu wa Ligi Kuu kwa ushindi wa mabao 2-1 dhidi ya Ihefu, Uwanja wa Sokoine,Mbeya.

Matokeo hayo yaliifanya Simba kuvuna pointi nne.

Biashara kwa upande wake, itashuka dimbani ikitoka kuvuna ushindi kwenye michezo yake yote miwili hivyo kuvuna pointi sita.

Timu hizo zilipokutana msimu uliopita, Simba iliibuka mbabe kwenye michezo yote miwili dhidi ya Biashara, ikianza kushinda mabao 2-0, dimba la Karume,  Musoma kabla ya kushinda mabao 3-1, Uwanja wa Mkapa, Dar es Salaam.

Hii ina maana kwamba, Simba itaingia uwanjani ikitaka kuendeleza ubabe, huku Biashara ikikusudia kufuta uteja.

Mchezo huo utakuwa wa kwanza kwa Simba kuchezwa kwenye uwanja wake wa nyumbani, hivyo itakuwa na shauku ya kupata ushindi ili kuwapa furaha wanazi wake.

Ili kuufanya uwanja huo kujaa mashabiki  wake, Simba ilitangaza kushusha kiingilio cha chini kutoka 5000 na kuwa 3000.

Kocha Mkuu wa Simba, Sven Vandenbroeck, alisema kuna faida nyingi ya kucheza uwanja wa nyumbani, amefanya maandalizi mazuri ya kucheza soka la kushambulia.

Alisema katika mchezo huo atamkosa Charles Ilafya ambaye amepewa ruhusa ya siku tatu kushughulikia matatizo ya kifamilia.

“Tunacheza nyumbani matarajio yetu ni kucheza vizuri na kutafuta ushindi, kiufundi tumefanya maandalizi   yatakayotupa matokeo mazuri,” alisema Sven.

Kwa upande wake Kocha Mkuu wa Biashara United, Francis Baraza, alisema anapanga kikosi  chaushindani kwa Simba kutokana na kufahamu ubora wa timu hiyo.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles