23.4 C
Dar es Salaam
Saturday, April 27, 2024

Contact us: [email protected]

Shabiki Azam afariki dunia Chamazi

Pg 32NA JENNIFER ULLEMBO, DAR ES SALAAM

SHABIKI wa Azam FC kutoka Tawi la Mpira Kazi lililopo Kiwalani, jijini Dar es Salaam, Emannuel Machide, jana alifariki dunia baada ya kukanyagwa na gari katika eneo la maegesho ya magari.

Tulio hilo la kusikitisha lilitokea ndani ya Uwanja wa Azam Complex uliopo Chamazi wakati mchezo wa Ligi Kuu Tanzania Bara kati ya Azam na Stand United ukiendelea.

Mashide ambaye alikuwa kwenye gari lililowabeba mashabiki wa Azam waliokuwa wakiingia uwanjani kushuhudia mchezo huo huku wakishangilia na kupiga ngoma, alianguka chini na kukanyagwa na gari ndipo umauti ukamkuta papo hapo.

Pamoja na kumpoteza shabiki wao katika mchezo wa jana, Azam waliendeleza kasi yao ya kuwania ubingwa wa Ligi Kuu msimu huu baada ya kuichapa Stand United ya Shinyanga bao 1-0.

Bao lililowapa ushindi wa pointi tatu Azam liliwekwa wavuni na beki Shomari Kapombe dakika ya 63 na kuiwezesha timu hiyo kufikisha pointi 50 sawa na Yanga wanaoshika nafasi ya pili wakitofautiana kwa wastani wa mabao ya kufungwa na kufunga.

Timu zote zilianza mchezo wa jana kwa kasi kwa kila mmoja kusaka bao la kuongoza, lakini Stand United ndio walikuwa wa kwanza kufanya shambulizi kali langoni kwa Azam dakika ya 23 kupitia kwa Frank Hamis lakini halikuzaa matunda.

Hamis alifanikiwa kumtoka mlinzi wa kimataifa wa Ivory Coast, Pascal Wawa na kuachia shuti kali ambalo liliokolewa na kipa wa Azam, Aishi Manula.

Kipindi cha kwanza kilimalizika kwa timu zote bila kufungana, hali iliyowafanya Azam kuanza kipindi cha pili kwa kufanya mabadiliko ya kumtoa mshambuliaji, Allan Wanga na kumwingiza John Bocco.

Mabadiliko hayo yaliwaongezea nguvu Azam na kufanikiwa kuandika bao la ushindi dakika ya 63 kupitia kwa Kapombe ambaye aliunganisha  mpira wa krosi ndefu iliyochongwa na Bocco.

Simba ndio vinara wa ligi hiyo kwa kujikusanyia pointi 54 baada ya kushuka dimbani mara 23 lakini Yanga wamecheza mechi 21 sawa na Azam wakiwa wamebakiwa na michezo miwili mkononi.

 

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles