Asha Bani – Dar es Salaam
BEI ya vyakula katika maduka na masoko mbalimbali jijini Dar es salaam, vimepanda hali inayosababisha walaji kulalamikia hali hiyo.
Vyakula hivyo ni pamoja na unga wa sembe, mchele ,viungo kama vile nyanya na vitunguu na hata nishati ya gesi kwa matumizi ya nyumbani.
Wakizungumza na MTANZANIA jana baadhi ya wananchi walisema kuwa hali hiyo ni lazima mamlaka zinazohusika zichukua hatua za haraka.
Akizungumzia hilo, mkazi wa mjini Songea mkoani Ruvuma, Arafa Faki alisema bei ya vyakula hata kwa wao wa mkoani nayo iko juu huku akitaja bei ya unga kilo moja Sh 1,500 wakati awali ilikuwa Sh 800 kwa kilo moja, mchele kilo moja Sh 2,200 , maharage kilo Sh 3,000 , vitunguu sado Sh 16,000 nyanya sado moja Sh 7,000.
“Yaani tulizoea kuona unga kilo moja shilingi 800,maharage kilo moja shilingi 1200 ,sado la nyanya 3000 mpaka 4000 lakini kwa sasa hali imebadilika na vitu vimepanda bei ghafla hadi huku wanapotokea wakulima wenyewe,’’ alisema Arafa.
Mkazi wa Tandika jijini Dar es Salaam, Tina Richard alisema maharage kilo Sh 2400, vitunguu kimo moja Sh 3,400 , nyanya sado Sh 9,000 na unga kilo moja Sh 2200.
“Sio vyakula tu jana ndio nilichoka nilipokwenda kununua Gesi ya kupikia nimekuta niliyokuwa nanunua na 48000 kwa sasa ni shilingi 54000 kila kitu kinapanda bei wakati umekuwa mgumu kwa kuwa ni vitu ambavyo ni lazima kuvitumia,’’alisema Tina.
Hali hiyo pia ipo katika masoko mbalimbali yenye kutoa huduma kwa jamii na yaliyokuwa yakitegemewa kwa Jiji la Dar es Salaa hasa ya Kariakoo, Kisutu, Buguruni.
Akitolea ufafanuzi kupanda kwa vyakula, Waziri wa Kilimo Japhet Hasunga alisema ni kweli na hali hiyo inatokana na usambazaji kuwa mdogo na hata hivyo kwa mikoa iliyomwandikia barua tayari wameanza kupelekewa mahindi kutoka ghala la taifa la mazao.
“Vyakula vimepanda bei kutokana na usambazaji umekuwa mdogo na mahitaji yamekuwa mengi lakini serikali imefanya utaratibu wa kusambaza mahindi kutoka ghala la Taifa la kuhifadhi chakula ila kwa mikoa ambayo imeandika maombi ya kutakiwa kufanyiwa hivyo,’’alisema Hasunga.
Alipoulizwa kuhusu Mkoa wa Dar es Salaam, kama wameandika maombi hayo alisema bado hawajaonesha kama wanauhitaji huo.