25.2 C
Dar es Salaam
Friday, April 26, 2024

Contact us: [email protected]

Polisi Morogoro yashikilia 32

Na Ashura Kazinja-Morogoro

WATU 32 wanashikiliwa na Jeshi la Polisi mkoani hapa kwa makosa tofauti ikiwemo kumiliki silaha kinyume na sheria, kukutwa na vitu vya wizi na bangi.

Akizungumza na waandishi wa habari jana, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Morogoro, Wilbroad Mutafungwa, alisema katika tukio la kwanza wanashikiliwa watu 16 kwa tuhuma za kuhusika na kushusha vitu kwenye magari, maarufu kama shushashusha katika Barabara ya Morogoro – Dar es Saalam.

Mutafungwa alisema msako mkali ulifanywa Agosti 16, majira kati ya saa saba usiku na saa 12 asubuhi baada ya kupata taarifa kutoka kwa wananchi wanaoishi maeneo ya Kingolwira, Mkambarani, Mikese na Pangawe wilayani Morogoro, ambayo yametokea matukio ya kushusha mizigo kutoka kwenye magari yanayosafiri kwenye barabara hiyo.

“Wamekamatwa watu 16 wakiwa na mali mbalimbali ndani ya nyumba zao, zilizopatikana kwa njia isiyo halali ambazo ni mifuko minne ya simenti, magodoro matatu, radio sita na spika zake, pikipiki mbili, televisheni nne, kanga doti 10, mipira ya gesi mitatu, tairi za pikipiki 12, turubai bando moja na rejeta moja ya gari,” alisema Mutafungwa.

Alivitaja vifaa vya kuvunjia na kufanyia uhalifu vilivyokamatwa ni spana, nyundo, tochi, bisibisi, visu na kofia za kuficha uso (Mask).

Hata hivyo alisema watuhumiwa wote wanaendelea kuhojiwa na kwamba upelelezi utakapokamilika watafikishwa mahakamani kujibu tuhuma zinazowakabili.

Aidha Mutafungwa alisema jeshi hilo linamshikilia Frank Mathias, mkazi wa Kijiji cha Madizini wilayani Mvomero kwa tuhuma za kumiliki bunduki aina ya gobole kinyume na sheria.

Katika hatua nyingine, Mutafungwa ametumia nafasi hiyo kutoa wito kwa wagombea wa nafasi mbalimbali katika Uchaguzi Mkuu ujao kutotumia maneno ya uchochezi wakati wa kampeni.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles