23.3 C
Dar es Salaam
Friday, April 26, 2024

Contact us: [email protected]

Nape kutoa tamko hukumu upangaji matokeo

NapePHOTOMWALI IBRAHIM NA ADAM MKWEPU, DAR ES SALAAM

WAZIRI wa Habari, Michezo, Sanaa na Utamaduni, Nape Nnauye, amesema anasubiri barua ya maamuzi yaliyotolewa na Kamati ya Nidhamu ya Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), juu ya shauri la upangaji wa matokeo ya kundi C Ligi Daraja la Kwanza ili atoe tamko lake kupitia hukumu iliyotolewa.

Katika maamuzi hayo, timu ya Geita Gold, JKT Oljoro na Polisi Tabora zilishushwa daraja hadi Ligi Daraja la Pili (SDL), wakati JKT Kanembwa ikishushwa hadi ligi ngazi ya mkoa, baada ya kushika nafasi ya mwisho kwenye kundi C.

Kamati hiyo pia imewafungia maisha kutojihusisha na soka mwamuzi wa mchezo kati ya JKT Kanembwa FC na  Geita Gold, Saleh Mang’ola na kamisaa wa mchezo huo, Moshi Juma, Kocha Msaidizi wa Geita, Choke Abeid na Mwenyekiti wa Chama cha Mpira wa Miguu  Tabora, Yusuph Kitumbo na Katibu wake, Fateh Remtullah.

Wengine ni  Mwenyekiti wa Klabu ya JKT Oljoro, Amos Mwita na Kocha Msaidizi wa Polisi Tabora, Bernard Fabian, huku makipa Mohamed Mohamed wa JKT Kanembwa na Dennis Richard wa Simba anayecheza kwa mkopo Geita Gold, wakifungiwa miaka 10 kutojihusisha na soka na kulipa faini ya Sh milioni 10 kila mmoja.

Akizungumza na MTANZANIA jana, Nape alisema bado hajapata nakala ya maamuzi hayo kutokana na kutokuwepo jijini hapa na pindi atakapoipata na kuipitia atatoa tamko lake.

“Nilisikia kuwa kuna kesi hiyo ya upangaji matokeo, lakini bado sijajua maamuzi yaliyotolewa na TFF, nipo nje kidogo ya mkoa, nitakaporudi na kupata nakala ya maamuzi hayo nitayapitia vizuri na ndipo nitatoa tamko,” alisema.

Kwa upande wake, Katibu Mkuu wa  Baraza la Michezo Tanzania (BMT), Mohamed  Kiganja, alisema watakuwa  tayari kuwasikiliza watakaolalamika kuonewa baada ya hukumu hiyo.

“Mimi nasikia tu kupitia vyombo vya habari, hivyo siwezi kutolea maoni hukumu hiyo, hadi inifikie ndio niweze kuzungumzia kwa kuwa  kila taasisi inaongozwa na taratibu zake za  kufanya kazi na kutekeleza majukumu  waliyojipangia.

“Hata hivyo, milango ipo wazi kwa wanaoona kwamba walionewa juu ya hukumu hiyo, kwa kuwa Baraza lipo kwa ajili yao,” alisema Kiganja.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles