27.2 C
Dar es Salaam
Monday, May 6, 2024

Contact us: [email protected]

Mfanyakazi NMB ahukumiwa jela kwa utakatishaji fedha

Na KULWA MZEE-DAR ES SALAAM


MFANYAKAZI wa Benki ya NMB, Mtoro Midole na mwenzake Daudi Kindamba wamehukumiwa kwenda jela jumla ya miaka 28 baada ya kupatikana na hatia kwa makosa ya wizi, utakatishaji fedha na kuisababishia benki hiyo hasara ya Sh 1,029,454,383.64.

Hukumu hiyo iliyoandaliwana Hakimu Mkazi Mwandamizi, Godfrey Mwambapa na kusomwa mbele ya Hakimu Mkuu, Wanjah Hamza ilitolewa jana na Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu.

Akisoma hukumu hiyo, Hakimu Wanjah aliamuru washtakiwa hao mbali na adhabu ya kifungo, pia walipe kiasi cha Sh 1, 029,454,383.64  ambacho wanadaiwa kusababisha hasara kwa NMB.

Mshtakiwa John Kikoka ambaye alikuwa miongoni mwa washtakiwa hao aliachiwa huru baada ya mashahidi 21 walioitwa na upande wa mashtaka kutoa ushahidi kwenye kesi hiyo ya jinai namba 118 ya 2014, kushindwa kuthibitisha mashtaka dhidi yake pasipo kuacha shaka.

Katika kesi hiyo, washtakiwa walikuwa wakikabiliwa na mashtaka 13 ya kula njama, wizi, kusababisha hasara na utakatishaji wa fedha ambayo kila mshtakiwa alikuwa akikabiliwa na mashtaka mawili.

Hakimu Wanjah akisoma hukumu hiyo, alisema washtakiwa Midole na Kindamba wamekutwa na hatia katika shtaka la wizi ambalo aliwahukumu kifungo cha miaka mitano jela kila mmoja.

Katika shtaka la kutengeneza miamala ya uongo, ambalo linamkabili  mshtakiwa Midole, Hakimu Wanjah alisema atatumikia kifungo cha miaka 10 jela.

Kwenye mashtaka ya utakatishaji wa fedha, Hakimu Wanjah alisema washtakiwa Midole na Kindamba wamekutwa na hatia katika shtaka moja moja, kati ya mawili mawili yanayowakabili, hivyo kila mmoja atalipa faini Sh milioni 500 ama kutumikia kifungo cha miaka mitano jela.

Katika shtaka la kuisababishia hasara ya Sh 1,029,454,383.64  benki ya NMB, mahakama iliamuru kila mshtakiwa kulipa faini ya Sh milioni tano ama kutumikia kifungo cha miaka mitano jela.

Midole, Kindamba na Kikoka walikuwa wanadaiwa kuwa kati ya Julai Mosi, 2007 na Julai 30, 2009 katika Jiji la Dar es Salaam walitenda makosa 13 ikiwamo kula njama, wizi, utakatishaji wa fedha na kusababisha hasara ya Sh 1,029,454,383.64 Mali ya benki ya NMB.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
587,000SubscribersSubscribe

Latest Articles