23.4 C
Dar es Salaam
Saturday, April 27, 2024

Contact us: [email protected]

MBOWE, MAALIM SEIF WATAKA JPM AWATIMUE WALIOSABABISHA AJALI


Alisema kutokana na ajali hiyo, inaonyesha Taifa halina maandalizi ya kutosha ya kukabiliana na ajali zinazotokana na vyombo vya usafiri wa majini.

“Mtakumbuka mwaka 1996 tulipoteza zaidi ya Watanzania 1,000 kwa ajali ya Mv Bukoba, ilipaswa kuwa funzo kwetu, lakini mwaka 2011 Meli ya Mv Spice Islander ilizama katika Bahari ya Hindi na zaidi ya watu wengine 2,000 walipoteza maisha.

“Mwaka 2012 Meli ya Staget nayo ilizama wakafa abiria mamia kwa mamia, lakini hatukujifunza, sasa jana kivuko kimezama  saa nane mchana, lakini mpaka saa 12 hakuna operesheni yoyote ya uokoaji ya watu wenye taaluma au vifaa vya kuokoa ambavyo vilikuwa vimefika katika eneo la ajali,” alisema.

Alisema watu waliokuwa wanahangaika kuokoa ni wavuvi wadogo wadogo, na kwamba hapakuwapo askari au wanajeshi.

Mbowe alikwenda mbali kwa kuhoji kipaumbele cha nchi, na hata kushangazwa na kauli iliyotolewa na upande wa serikali ya kusitisha zoezi la uokoaji kwa sababu ya giza.

“Kweli tumeshindwa kuwa na taa ya kuokolea watu umbali wa mita 100 kutoka nchi kavu? Tumeshindwa hata kutumia jenereta la kawaida kwa kuipakia kwenye mtumbwi  kisha watu wawashe umeme na kuwamulikia wanaofanya kazi ya kuokoa? Ina maana hapo waliridhika kwamba wote waliokuwa majini wamekufa? Kweli hili jambo linaumiza sana,” alisema Mbowe.

Aliongeza kuwa, nchi haina huduma za uokoaji wa haraka katika maziwa yote makubwa na baharini.

MAALIM SEIF

Naye Katibu Mkuu wa Chama Cha Wananchi (CUF), Maalim Seif Sharif Hamad, amesema amepokea kwa masikitiko taarifa ya ajali hiyo na kutoa pole kwa Rais Dk. John Magufuli.

“Huu ni msiba wetu sote kama Taifa, pia nawapa pole ndugu, jamaa na wapendwa wote waliopoteza ndugu zao katika ajali hii, Mwenyezi Mungu awape subra katika kipindi hiki kigumu cha maombolezo ya kuondokewa na wapendwa wao.

“Tunawaombea marehemu wote Mwenyezi Mungu awasamehe makosa yao na kuwaingiza peponi, aidha, tunawaombea majeruhi wote waweze kupona haraka,” alisema Maalim Seif.

Maalim Seif pia alisema amesikitishwa na taratibu mbaya za uokoaji na hasa baada ya kusitisha zoezi nyakati za usiku kwa kukosekana mwanga.

“Sote tunafahamu kuwa ajali inaweza kutokea nyakati zozote zile, iwe usiku au mchana, ni wajibu wa mamlaka husika kuwa na maandalizi ya kutosha kwa kazi hizo, katika mazingira hayo iliwezekana kabisa kupata taa za dharura na vyombo vyenye taa vya uokozi ili kazi iweze kuendelea kwa wakati wote,” alisema Maalim Seif.

Alisema mkoani Mwanza kuna vikosi vya Jeshi, boti za doria za polisi, helikopta na vivuko vingine katika ziwa hilo.

“Ni kweli kuwa havina taa kubwa za kuwezesha zoezi la uokozi kuendelea usiku kucha? Huu ni msiba mkubwa kwa Taifa, ni wajibu wa serikali kuhakikisha kuwa inakomesha uzembe wa aina hii usiweze kujirejea tena kwa kuweka vipaumbele vya Taifa kwa kujali uhai na maisha ya Watanzania kwanza,” alisema Maalim Seif.

Alisema CUF inawataka viongozi wote wanaohusika na kadhia hii, wakiwamo mawaziri wa wizara husika kuwajibika kwa kujiuzulu nafasi zao au kuwajibishwa na mamlaka za uteuzi wao kwa kutochukua tahadhari ya mapema pamoja na Mbunge wa Ukerewe kutoa tahadhari hiyo ndani ya Bunge mara kadhaa.

Alisema kutozingatia angalizo la Mbunge wa Ukerewe kwa wakati mwafaka ni kitendo cha dharau kubwa na kuupuza uhai na maisha ya wananchi.

LOWASSA

Kwa upande wake, Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa, amesema amepokea kwa mshtuko taarifa ya ajali ya  kuzama kwa kivuko cha Mv Nyerere.

Lowassa aliyasema hayo kupitia taarifa fupi iliyotumwa na Msemaji wake, Aboubakar Liongo.

“Nawapa pole ndugu wote waliopoteza maisha, Mkuu wa Mkoa wa Mwanza na Watanzania wote kwa ujumla, huu ni msiba wa nchi nzima,” alisema Lowassa, ambaye pia ni mjumbe wa Kamati Kuu ya Chadema.

Alisema kwa sasa kama Taifa ni lazima kujiuliza na kujipanga ili kuhakikisha maafa kama hayo hayatokei tena, kwakuwa yanapoteza maisha ya wananchi wengi.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles