BARCELONA, HISPANIA
MAMILIONI ya wakazi wa Catalonia wameandamana jana katika mitaa ya eneo hilo kulalamikia ukiukwaji mkubwa wa haki za binadamu ulioshuhudiwa wakati wa kura ya maoni wiki iliyopita.
Hispania imeitaja kura hiyo ya maoni kuwa ni kinyume cha sheria japo zaidi ya watu milioni 2.2 walipiga kura.
Lakini mamia ya watu walijeruhiwa wakati polisi wa Hispania walipokuwa wakijaribu kuzuia zoezi hilo kuendelea.
Baadhi ya maofisa walioamrishwa kuwazuia watu wasipige kura, walionekana wakifyatua risasi za mipira, wakivamia vituo vya kupigia kura na kuwavuta nywele wanawake.
Maandamano hayo ya jana yalisababisha kufungwa kwa barabara kubwa, baa, maduka, migahawa, huku pia milango ya ofisi za serikali ikiwa imewekewa vizuizi.