23.4 C
Dar es Salaam
Saturday, April 27, 2024

Contact us: [email protected]

Majaji wa Escrow kitanzini

Hussein KatangaNa Kulwa Mzee, Dar es Salaam

TUME ya Utumishi wa Mahakama imesema suala la majaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania wanaotuhumiwa kupokea zaidi ya Sh milioni 400 kutoka katika Akaunti ya Tegeta Escrow, limefika kwenye tume hiyo na linafanyiwa kazi.
Kwa utaratibu wa tume hiyo, baada ya uchunguzi taarifa hupelekwa kwa rais ambaye baada ya kupitia mapendekezo yaliyotolewa kwenye ripoti ya uchunguzi, hutoa uamuzi.
Hayo yalielezwa jana na Mtendaji Mkuu wa Mahakama, Hussein Katanga, katika banda la Tume ya Utumishi wa Mahakama katika maonyesho ya Wiki ya Sheria yanayoendelea kwenye viwanja vya Mnazi Mmoja, Dar es Salaam.
“Suala la majaji waliohusishwa katika Escrow limeshaletwa katika tume. Lipo na taratibu zinaendelea,” alisema Katanga.
Majaji wanaotuhumiwa kuingiziwa fedha hizo ni Profesa Eudes Ruhangisa (Sh milioni 404.25) na Aloysis Mujulizi (Sh milioni 40.4).
Katanga alisema dawa ya kumaliza mambo ni kuwa wazi kusema.
“Huo ni ukweli, inatakiwa uwepo uwazi zaidi…Tunatakiwa kuwa wazi, hivi sasa tunataka kuweka mabango wananchi wajue jinsi ya kupata haki kuepusha rushwa,” alisema.
Akizungumzia hilo, Mkurugenzi Msaidizi wa Mahakama za Mwanzo, Warsha Ng’humbu, aliyekuwapo katika banda la Kurugenzi ya Ukaguzi, Malalamiko na Maadili, alisema kwa kuwa suala hilo limefika kwenye tume, maana yake lilishapita katika Kamati ya Maadili ya Majaji.
Katibu Msaidizi wa Tume ya Utumishi wa Mahakama, Enzeel Mtei, alisema tume hiyo inaundwa na wajumbe sita na ina jukumu la kumshauri rais juu ya uteuzi wa Jaji Kiongozi au majaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania.
Wengine ni Mtendaji Mkuu wa Mahakama, Msajili Mkuu, Msajili wa Mahakama ya Rufani na Msajili wa Mahakama Kuu au kutokuwa na uwezo kwa watendaji hao.
Majukumu mengine ni kuchambua malalamiko dhidi ya majaji na kuchukua hatua za utawala dhidi ya Jaji wa Mahakama ya Rufani, Jaji Kiongozi au jaji na hatua zilizoainishwa katika Katiba.
Alisema kwa majaji wanaokwenda kinyume na maadili, tume hiyo inachunguza madai hayo na kupeleka mapendekezo kwa rais kwa ajili ya uamuzi.
Mtei alisema tuhuma zinazoelekezwa kwa mahakimu wa wilaya na mkoa zinashughulikiwa na kamati ya mkoa na mahakimu wa mahakama za mwanzo tuhuma zao zinashughulikiwa na kamati ya wilaya.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles