25.2 C
Dar es Salaam
Friday, April 26, 2024

Contact us: [email protected]

Maalim Seif: Kazi imeanza

ASHA BANI Na KHAMIS SHARIF-dar / ZANZIBAR

SASA kazi imeanza. Ni kauli ya aliyekuwa Katibu Mkuu wa CUF, Maalim Seif Sharif Hamad, ambaye amesema kuwa wameanza kazi ya kukitangaza chama chake kipa cha ACT-Wazalendo nchi

nzima.

Maalim Seif amewataka wanachama wa CUF waliomfuata ACT-Wazalendo kumuunga mkono kutokatishwa tama na kauli za baadhi ya watu ikiwamo kubezwa.

Akizungumza na MTANZANIA jana Dar es Salaam wakati akielekea Zanzibar

ambako leo atakuwa na shughuli maalumu ya kujitambulisha kwa wananchi

baada ya kujiunga na ACT-Wazalendo, alisema kwa sasa kazi ya kukitangaza

chama hicho itafanyika nchi nzima -Bara na Visiwani.

“Watachokozwa sana, wasikubali kuchokozwa, sisi tuna hoja, waendelee kutuunga mkono, sisi tuna hoja.

Matarajio ya wale waliotuunga mkono waendeleena sisi kwa kila hali,” alisema Maalim Seif.

Baada ya kumaliza kuzungumza na MTANZANIA, Maalim Seif aliingia katika meli akiambatana na walinzi wake pamoja na aliyekuwa Naibu Katibu Mkuu wa CUF Zanzibar, Nassoro Ahmed Mazrui na Naibu Katibu Mkuu wa Chadema Zanzibar, Salum Mwalimu.

Awali asubuhi akiwa katika mahojiano na mtangazaji Maria Sarungi wa Kwanza Tv, Maalim Seif alisema kabla ya kuhamia ACT-Wazalendo walifanya tafiti katika vyama vinne.

Alivitaja vyama hivyo kuwa ni Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), NCCR-Mageuzi, NLD na ACT Wazalendo yenyewe ambayo amedai ndiyo iliyokidhi vigezo walivyovihitaji na kisha kuhamia.

Maalim Seif alisema walijenga urafiki kwa vyama hivyo huku wakiendelea na utafiti wao.

“Tulikuwa na vyama hivyo vinne, vitatu vilikuwa wenzetu katika Ukawa, ambao ni hao Chadema, NCCR-Mageuzi na NLD. ACT hawakuwa wanachama wa Ukawa (Umoja wa Katiba ya Wananchi), lakini walikuwa wameshaleta maombi ya kujiunga Ukawa.

“Tuliunda timu ya viongozi wetu na wote walikaribishwa kwa kila chama. Swali lilikuwa ni kwamba ikitokea sisi tunahama chama je, mtatukaribisha?

“Wote walisema karibuni, lakini tulikuwa na ‘criteria’ zetu. Je, malengo yetu na yao yanafanana? Baada ya kupima vigezo vyote hivyo, ni uamuzi uliokuwa

mgumu kidogo, lakini tukaona chama ambacho kimeanza kuaminika na wananchi hata kama ni kidogo tukachagua ACT-Wazalendo, katika vizuri basi kuna kizuri zaidi…” alisema Maalim Seif.

CHADEMA YAMTAMANI

Chama cha Chadema kimesema kilitamani kumchukua Maalim Seif, lakini hawakufikia makubaliano, hata hivyo wameamua kushirikiana naye katika

chama chake kipya cha ACT Wazalendo.

Maalim Seif alikuwa mmoja wa wanasiasa waliounga mkono kwa nguvu zote uamuzi wa vyama vinne vilivyounda Ukawa kumuunga mkono Edward Lowassa aliyeteuliwa na Chadema kugombea urais.

Akizungumza na waandishi wa habari Dar es Salaam jana, Naibu Katibu Mkuu wa Chadema Zanzibar, Mwalimu, alisema pamoja na kumkosa Maalim Seif

na kundi lake, wataendelea kushirikiana naye kwa kuzingatia mkutano wa vyama vya upinzani uliofanyika Zanzibar Desemba mwaka jana.

Mwishoni mwa mwaka jana, Baraza la Wazee la Chadema lilitangaza kumkaribisha Maalim Seif katika chama hicho wakati mgogoro wa CUF ukishika kasi.

“Hakuna pigo, tulimtaka kweli. Viongozi wetu kwa hekima na busara

waliona huyu mtu akija huku ni jambo jema na sisi tuliona tunusuru hadhi na heshima yake na mapambano ya demokrasia.

“Sasa kama amekwenda kwa mwenzio, ndugu yangu hajaolewa binti yako

ameolewa binti wa baba mdogo, sasa si mulemule?

“Kama ni tajiri utashindwa kwenda kuomba chakula? Maana una binti na

mdogo wako ana binti, hajaolewa wako kaolewa wa ndugu yako, hayo si mulemule? Hutahudhuria sherehe?” alisema Mwalimu.

Kuhusu mipango ya Chadema Zanzibar, Mwalimu alisema wataendelea na programu zao, lakini hawatapambana na ACT-Wazalendo.

HEKAHEKA UNGUJA

Siku moja baada ya Maalim Seif kuhama CUF na kujunga na ACT- Wazalendo,

harakati za kukua na kuendelea kwa kasi kwa chama hicho visiwani Zanzibar

zimepamba moto.

Hatua hiyo imekwenda sambamba na ofisi za matawi ya CUF kubadilishwa rangi na kupakwa rangi za ACT- Wazalendo pamoja na kupandishwa kwa bendera za chama hicho.

Sambamba na hayo, wanachama waliomuunga mkono Maalim Seif jana walikuwa kwenye shamrashamra kwa kunywa kahawa na haluwa za bure hasa katika maeneo ya Mji Mkongwe.

MTANZANIA pia ilishuhudia wanachama hao wapya wa ACT- Wazalendo wakichinja mbuzi na kuku huku damu zikitapakaa katika maeneo hayo ikiwa ni ishara ya furaha.

Akizungumzia matukio hayo, aliyekuwa Katibu wa CUF Jimbo la Malindi, Ahmed Bashuti, alisema shamrashamra hizo zitakuwa endelevu katika matawi yote ya jimbo hilo.

Alisema baada ya kupita katika misukosuko katika chama cha zamani – CUF, wameona ni vema kufanya tafrija kwani wananchi wa Zanzibar walikuwa

kifungoni.

Pamoja na hali hiyo, baadhi ya waliokuwa wanachama wa CUF, walisema kwa sasa wana hofu kuwa mali za chama hicho huenda zikasambaratika kwa kuhodhiwa na mtu mmoja.

Mmoja wa wanachama wapya wa ACT-Wazalendo, Kassim Ali (50), alidai

kuwa Profesa Ibrahim Lipumba hakuwa na nia njema na CUF.

Alidai kitendo cha Profesa Lipumba kuacha mapambano wakati wa Uchaguzi

Mkuu mwaka 2015 na baadaye kurudi, ni ishara tosha kuwa alikuwa na kazi

yake maalumu ambayo sasa anakwenda kukimaliza chama hicho.

Hata hivyo madai hayo yalipingwa na Profesa Lipumba katika mkutano

wake na wanahabari juzi Dar es Salaam, akisema kuwa Maalim Seif alikuwa anataka kujenga usultani ndani ya CUF jambo ambalo katu halikubaliki.

Mjumbe wa zamani wa Baraza la Wawakilishi (BLW), Jimbo la Micheweni, Thubeit Khamis, alipoulizwa kuhusumajengo ya CUF kugeuzwa kuwa ofisi za

ACT-Wazalendo, alisema ni haki yao kufanya hivyo kwani majengo mengi ni nyumba za watu wamejitolea kwa chama.

Naye aliyekuwa Katibu wa CUF Wilaya ya Chakechake Pemba, Saleh Nassor Juma, alisema walipokea maagizo kutoka kwa uongozi wa juu ambao uliwataka waanze kubadilisha rangi na bendera za matawi yao.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles