29.3 C
Dar es Salaam
Thursday, May 2, 2024

Contact us: [email protected]

DC AHIMIZA WANAWAKE KUNYONYESHA

Na JUDITH NYANGE


Mother nursing son

MKUU wa Wilaya ya Nyamagana mkoani Mwanza, Mary Tesha, amewasihi wanawake  wote wanaojifungua kunyonyesha watoto wao kwa miezi sita bila kuchanganya na kitu kingine chochote.

Alisema hiyo ni kwa sababu  maziwa ya mama yana virutubisho muhimu kwa ukuaji wa watoto wao.

Alikuwa akizungumza jana wakati wa hafla ya kupokea msaada wa katoni  mbili za maziwa  kwa ajili ya  watoto wanaoshindwa kunyonya kutokana na matatizo mbalimbali.

Msaada huo ulitolewa na Kampuni ya Twincity   katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Mwanza,  Sekou Toure.

Alisema maziwa ya mama yana virutubisho vya vitamin, calcium   na vingine vingi ambavyo vinasaidia  katika ukuaji wa motto.

DC alisema  ndiyo maana wataalamu wa afya wanashauri motto anyonyeshwe mpaka atakapotimiza miezi sita bila kulishwa kitu kingine kama mama hana tatizo lolote la  afya.

“Wapo baadhi ya wazazi ambao wanajifungua na kuogopa kunyonyesha kwa kuhofia maziwa yao kulala na kuanza  kuwapa watoto wao maziwa ya ng’ombe.

Maziwa ya ng’ombe  ni rahisi kuwa na vijidudu vinavyoweza kusababisha magonjwa  mbalimbali na kumfanya mtoto kudhoofu kwa kukosa lishe bora.

“Kwa mujibu wa ripoti ya utafiti uliotolewa na shirika  lisilo la kiserikali la Save the Children, watoto 300 chini ya umri wa miaka mitano  hufariki dunia   kila siku kutokana na magonjwa yanayosababishwa na  ukosefu  wa lishe na asilimia 42 hudumaa kutokana na tatizo hilo,”alisema Tesha.

Alisema inasikitisha kuona mtoto ambaye  anabaki  baada ya mama yake  kufariki dunia wakati wa kujifungua anakua  kwa  kukosa  lishe ambayo angeipata kwa kunyonya maziwa ya mama yake.

Tesha alisema changamoto za upungufu wa lishe husababishwa  na mambo mbalimbali ikiwamo watoto kuzaliwa na tatizo la mdomo sungura, kujifungua kwa upasuaji  na wazazi kufariki dunia   baada ya kujifungua na hivyo watoto wao kushindwa kunyonya vizuri.

Matatizo mengine ni mama kukosa maziwa,  kuugua muda mrefu na hivyo kulazimika kuwaacha watoto wao nyumbani kwa kuepusha kupata maradhi yanayotokana na mazingira ya  hospitali na kusababisha kukosa maziwa ya mama na kupata matatizo ya ukosefu wa lishe.

Aliwataka  wazazi  wanaopatiwa maziwa hayo wayatumie kama ilivyokusudiwa kwa sababu wapo baadhi  wanahisi wana mahitaji zaidi ya maziwa na hivyo kuyauza ili  watatue matatizo mengine yanayowakabili.

Meneja Masoko wa Kampuni ya Twincity, Nina Kimaro,  alisema maziwa hayo yana virutubisho vyote muhini na  ni kwa ajili ya watoto kutoka kuzaliwa mpaka mwaka mmoja ambao wanakabiliwa na matatizo mbalimbali ikiwamo kupoteza wazazi au kuzaliwa na tatizo la mdomo sungura na hivyo kushindwa kunyonya maziwa ya mama zao.

Mmoja wa waliopatiwa msaada huo,  Ester Kasela, alishukuru kwa msaada huo pamoja na Serikali kwa kuendelea  kujali afya ya mama na mtoto  na kuendelea kuwaboreshea huduma zao katika vituo vya afya , zahanati na hospitali zote nchini ili kupunguza vifo vinavyotokana na uzazi.

“Sekou Toure ile ya zamani siyo ya leo…huduma nilizoziona  zinatolewa leo hapa mimi kama mzazi naushukuru uongozi na wauguzi.

“Tangu nimefika hapa nakaribia kumaliza wiki lakini sijamuona mzazi au mtoto aliyefariki, hii inaonyesha jinsi wauguzi wanavyojali afya ya mama na mtoto,” alisema Kasela.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles