29.3 C
Dar es Salaam
Thursday, May 2, 2024

Contact us: [email protected]

KIGWANGALA AMWAJIBISHA TABIBU

Na SHOMARI BINDA


NAIBU Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Ustawi wa Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Dk. Hamis Kigwangala ameagiza kusimamishwa kazi, tabibu wa Kituo cha Afya Kiagata wilayani Butiama.

Tabibu huyo, Mtatiro Daniel amesimamishwa kutokana na kutumia stakabadhi bandia kukusanya Sh milioni mbili  za Mfuko wa Afya ya Jamii (CHF) zilizochangwa na wananchi.

Dk. Kigwangala alisema licha ya kusimamishwa kazi, tabibu huyo anastahili kuwa mikononi mwa  vyombo vya dola,   Jeshi la Polisi na Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) ambavyo vinapaswa kuchukua hatua zinazostahili kwa mujibu wa sheria.

Dk. Kigwangala alitoa agizo hilo muda mfupi baada ya kufanya ziara ya kushtukiza kwenye kituo hicho cha afya na wananchi kumlalamikia tabibu huyo kwa kukusanya fedha kwa stakabadhi bandia.

Alisema taratibu za ukusanyaji wa fedha kwa ajili ya kuchangia mfuko wa CHF unafahamika na wananchi wanaujua.

Naibu waziri alisema  kitendo cha kukusanya fedha bila utaratibu hakiwezi kukubalika na watumishi wa namna hiyo wanapaswa kuchukuliwa hatua.

Alisema vyombo vya dola vinapaswa kulichunguza suala hilo na  atakapobainika kufanya hivyo kwa ajili ya kujinufaisha achukuliwe hatua ili iwe fundisho kwa watumishi wengine wa kada ya afya wanaofanya vitendo kama hivyo.

“Huu siyo utaratibu na nichukue nafasi hii kuwashukuru wananchi kwa kutoka kimya na kutoa taarifa juu ya vitendo ambavyo vinakwenda kinyume na utaratibu mahali popote panapotolewa huduma za afya.

“Ni ubadhirifu ambao ulikuwa unatendeka hapa na wananchi wametueleza wazi hivyo vyombo vya dola fanyeni kazi yenu kwa kufuatilia jambo hili na  ukweli utakapobainika chukueni hatua,” alisema.

Akiwa kwenye ziara yake mkoani Mara, Naibu Waziri  pia alitembelea Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Mara na Kituo cha Afya cha Nyasho kilichopo Manispaa ya Musoma.

Aliahidi kuzifuatilia changamoto mbalimbali zinazokabili huduma ya afya.

Mkuu wa Wilaya ya Musoma, Dk. Vicent Naano, alisema ziara ya Naibu Waziri imekuwa chachu ya kutekeleza na kutoa  huduma za afya kwa wananchi.

Alisema  yapo maeneo ambayo wananchi wamekuwa wakilalamika huduma  zinatolewa, malalamiko ambayo hayana budi kutafutiwa ufumbuzi.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles