32.2 C
Dar es Salaam
Monday, May 13, 2024

Contact us: [email protected]

CCM Simiyu yakemea wajawazito kudaiwa fedha huduma za afya

Na Samwel Mwanga, Itilima

MWENYEKITI wa Chama Cha Mapinduzi(CCM) Mkoa wa Simiyu, Shemsa Mohammed amehaidi kulivalia njuga suala la baadhi ya wahudumu wa Afya katika Wilaya ya Itilima mkoani humo wanaodaiwa kuwatoza fedha wanawake wajawazito ili waweze kupata kadi ya mahudhurio yao ya kiliniki.

Pia, amesema Sera ya Taifa ya Afya inataka huduma za afya ya uzazi kwa wajawazito na watoto chini ya umri wa miaka pamoja na wazee wenye umri kuanzia miaka 60 zinatolewa bure lakini bado kwa wajawazito wanatakiwa kulipia katika baadhi ya zahanati katika Wilaya ya Itilima.

Amesema hayo Aprili 27, mwaka huu katika kijiji cha Laini wakati akisikiliza na kutatua kero kwa wanachama wa chama hicho na wananchi wa Tarafa ya Bumela mara baada ya wananchi kutoa malalamiko hayo mbele yake.

Amesema kuwa katika Ilani ya CCM ya mwaka 2020-2025 imeeleza kuwa wajawazito, watoto chini ya miaka mitano na wazee wenye umri wa kuanzia miaka 60 watapatiwa huduma bure za afya katika zahanati, vituo vya afya na zahanati za Serikali lakini bado katika wilaya hiyo wajawazito wanatozwa fedha kupata huduma za afya jambo hilo halikubaliki hata kidogo.

Mwenyekiti wa Wazee katika Kijiji cha Laini wilayani Itilima,Masumbuko Langa akieleza kero yake mbele ya Mwenyekiti wa CCM mkoa Simiyu, Shemsa Mohamed(hayupo pichani).

“Serikali inayoongozwa na Mwanamama shupavu, Dk. Samia Suluhu Hassan ilishaweka utaratibu wa utoaji wa huduma za afya kwa wajawazito,watoto chini ya miaka mitano na wazee wenye umri kuanzia miaka 60 lakini hapa wilaya ya Itilima bado wajawazito wanatozwa Sh 5,000 kwa ajili ya kadi za kiliniki hili jambo halikubaliki hata kidogo wakati kadi hizo zinatolewa bure.

“Ninasikitika kuona hata wazee hawapewi huduma za afya najua Mkuu wa wilaya umeshapokea malalamiko hayo na umehaidi utalifanyia kazi naomba awamu nyingine ninapokuja kufanya ziara katika wilaya hii hizi kero ndogondogo zilizomo ndani ya uwezo wenu mnazitatua si hadi tuje sisi kutoka mkoani,” amesema Shemsa.

Mwenyekiti huyo amewataka watumishi wa sekta ya Afya katika mko huo kufanya kazi zao kwa kufuata taratibu zilizowekwa na ambaye anao hawezi ni vizuri akatafuta mkoa mwingine wa kufanyia kazi za si mkoa huo wa Simiyu kwani hawezi kuwavumilia .

“Wakati niko hapa nimeelezwa kuwa zahanati ya Laini haifanyi kazi kwa kuwa watoa huduma walioko hapo ambao ni wawili wamefunga zahanati kwenda kwenye msiba hili jambo hili halikubaliki maana ugonjwa hauna hodi unakuja wakati wowote niwaombe watumishi wa sekta ya afya katika mkoa wa Simiyu tufuata taratibu zetu za kazi ambaye hawezi basi atupishe katika mkoa wetu,”amesema.

Mkuu wa Wilaya ya Itilima mkoani Simiyu, Anna Gidarya akijibu hoja katika Mkutano wa kusikiliza kero za wananchi katika Tarafa ya Bumela ulioitishwa na Mwenyekiti wa CCM Mkoa wa Simiyu, Shemsa Mohammed(hayupo pichani).

Naye Mkuu wa Wilaya ya Itilima, Anna Gidarya amekiri kuwepo kwa malalamiko hayo kwa baadhi watoa huduma za afya katika wilaya hiyo na kuwa tayari amekwishaa anza kuyafanyia kazi kwani serikali inafanya kazi kubwa sana ya kuboresha huduma za afya ikiwemo miundo mbinu na vifaa tiba pamoja na dawa.

“Nimeshaongea na DMO (Mganga Mkuu wa Wilaya) wa Itilima aniletee orodha ya watumishi wa sekta ya afya ambao hawatekelezi majukumu yao kwa wananchi ili nilinganishe na orodha yangu niliyonayo niliyoipata kwa kutumia njia zangu ili niweze kuchukua hatua ,” amesema Anna.

Mwakilishi wa Mganga Mkuu wa Wilaya ya Itilima, Oswin Mlelwa amesema kuwa wamekuwa wakiwaelekeza watumishi wote wa sekta ya Afya katika wilaya hiyo kuhakikisha wanatoa huduma muda wote na vituo vyote vya afya kuanzia zahanati vinakuwa wazi kwa muda wa masaa yote ili wananchi waweze kupata huduma.

“Kila mara tunawakumbusha watumishi wa idara ya afya katika wilaya yetu wasifanye kazi kwa mazoea na vituo vyetu vyote vitoe huduma kwa masaa yote na pia tulishazielekeza serikali za vijiji ziweze kuwatambua wazee wenye umri wa miaka 60 ili waweze kupata huduma bure za afya,” amesema.

Awali, Samwel Mbabani, ambaye ni mkazi wa kijiji cha Sagata ameeleza kuwa wauguzi katika zahanati ya Sagata hawatoi huduma nyakati za usiku na hali ambayo ilipelekea Mke wake kujifungulia kwenye nje ya zahanati hiyo.

Sehemu ya Wananchi waliojitokeza katika mkutano wa kusikiliza kero za wananchi katika Tarafa ya Bumela uliofanyika kwenye Kijiji cha Laini wilaya ya Itilima mkoa wa Simiyu.

Mwenyekiti wa wazee katika Kata ya Laini.Masumbuko Langa amesema kuwa ni vizuri serikali ikasimamia sera yake ya kuwapatia matibabu bure wazee kwani wamekuwa hawapati huduma hiyo na kuona hana umuhimu wa kuwa na wadhifa huo katika kijiji hicho.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
587,000SubscribersSubscribe

Latest Articles