27.2 C
Dar es Salaam
Thursday, May 2, 2024

Contact us: [email protected]

Bares kulamba mkataba mpya JKT Tanzania

NA MOHAMED KASSARA

-DAR ES SALAAM

KLABU ya JKT Tanzania ipo katika hatua za mwisho za kumsainisha mkataba mpya kocha wa timu hiyo, Mohamed Abdallah ‘Bares’, kwa ajili ya kuendelea kukinoa kikosi hicho msimu ujao  wa Ligi Kuu Tanzania Bara.

JKT Tanzania umefikia hatua hiyo, baada ya kuridhishwa na uwezo wa kocha huyo aliyeisadia timu kubaki Ligi Kuu, baada ya kuandamwa na mfululizo wa matokeo mabaya uliosababisha timu hiyo kujiweka katika hatari ya kushuka daraja.

Timu hiyo inayomilikiwa na Jeshi la Kujenga Taifa(JKT)ilimaliza msimu katika nafasi ya 10 miongoni mwa timu 20, ikiwa na pointi 47, baada ya kushuka dimbani mata 38, ikishinda 11, sare 14 na kuchapwa mara 13.

Bares kabla ya kuinoa JKT Tanzania, alikuwa kocha wa Tanzania Prisons lakini alipigwa chini kwa kile kilichoelezwa mwenendo mbaya wa timu hiyo.

Alijiunga na JKT Tanzania akichukua nafasi ya Bakari Shime aliyesimamishwa siku chache baada ya timu hiyo kupokea kichapo cha mabao 6-1 kutoka kwa Azam FC.

Baada ya kuchukua jukumu hilo, Bares alifanya kazi kubwa ya kuiokoa timu hiyo kutoka shimoni na kuinusuru kuteremka daraja, licha ya kuikuta kwenye hali mbaya, huku ikiwa imebakiza michezo michache kabla ya msimu kumalizika.

 Akizungumza na MTANZANIA jana, Bares alikiri kuwa mbioni kusaini mkataba mpya wa kuendelea kuifundisha timu hiyo, baada ya uongozi kuona kazi kubwa aliyoifanya katika kikosi hicho alichokinoa kwa mwezi mmoja.

Alisema mazungumzo kati yake na uongozi wa timu hiyo yanaendelea vizuri na muda wowote kuanzia sasa atasaini mkataba mpya na kuzima tetesi zilizokuwa zimezagaa kuwa ataikacha  timu hiyo.

“Ni kweli kabisa uongozi umeniita na kunieleza nia yao ya kunipa mkataba mpya wa kuendelea kusalia hapa, nafikiri wameona kazi niliyoifanya msimu ulioisha hivi karibuni, mpira ni kazi yangu, hivyo naendelea kusikizia ofa yao kama itanifaa basi nitasaini.

“JKT Tanzani ni timu nzuri, hivyo  ni furaha kwangu kuona bado natakiwa kubaki, naendelea kuangalia mwelekeo wa mazungumzo kati yangu na uongozi, nataka mkataba ambao utakuwa na usawa kwa pande zote, sina tatizo kufanya nao kazi, ila lazima nao wasikilize matakwa yangu, tukifikia makubaliano nitasaini,”alisema kocha huyo wa zamani wa JKU ya Zanzibar.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles