23.1 C
Dar es Salaam
Wednesday, May 8, 2024

Contact us: [email protected]

Barakoa kila kona

 AVELINE KITOMARY Na RAMADHAN HASSAN – DAR/DODOMA

KUANZIA leo wananchi wa Jiji la Dar es Salaam, huenda wakajikuta wakikwama kupata huduma kutokana na kutakiwa kuvaa barakoa kama njia ya kujinga na maambukizi ya virusi vya homa kali ya mapafu (Covid-19) ambavyo husababisha ugonjwa wa corona.

Pamoja na hali hiyo, pia wametakiwa kuchukua hahadhari ya kujikinga na ugonjwa huo, huku idadi ya wagonjwa ikiongezeka na kufikia 170 baada ya kuongezeka wagonjwa wapya 23 kutokea Visiwani Zanzibar.

Hatua ya uvaaji wa barakoa, inatokana na agizo lilotolewa na Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda mwishoni mwa wiki iliyopita.

Makonda alisema kuanza leo, wakazi wote hawataruhusiwa kutoka kwenda popote wala kupanda daladala bila kuvaa barakoa (mask).

Pamoja na hilo, pia aliagiza bishara zote zianze kufanyika kwa njia kufunga (take away).

Kutokana na agizo hilo saa chache masharika na taasisi za umma, zikiwamo hospitali nazo zilitoa matangazo ya kuwataka watu waote wanaokwenda kupata huduma kuvaa barakoa na asiyevaa hatoruhusiwa kuingia ndani kuhudumiwa.

Hatua hiyo, inatajwa kama njia ya kudhibiti maambukizi hayo ambapo kwa sasa Dar es Salaam inaongoza kwa kuwa na idadi kubwa ya maambukizi, huku ikifutiwa Zanzibar.

WAZIRI HAMADI

Jana Waziri wa Afya wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ), Hamadi Rashid Mohamed, alitoa taarifa na kusema idadi ya wagonjwa visiwani humo imefikia 58 kutoka 35 ya awali, kesi mpya ni 23 zimebainika.

Katika taarifa hiyo, Hamad alisema idadi ya vifo vinavyotokana na ugonjwa huo, imeongezeka kutoka vifo vitatu hadi saba.

Kwa mujibu wa taarifa ya mwishoni mwa wiki, Tanzania ilikuwa na wagonjwa 147 ambapo kwa ongezeko la wagonjwa wapya 23 inafanya nchi kuwa na wagonjwa 170.

“Wizara ya Afya Zanzibar , inatoa taarifa ya ongezeko la wagonjwa wapya 23 wa corona na kufanya idadi ya wagonjwa Zanzibar kufikia 58 kutoka wagonjwa 35 ambao tuliwatolea taarifa Aprili 17, mwaka huu.

“Kati ya wagonjwa wapya,21 wanaishi Unguja na wawili wanaishi Pemba, kati ya hao wagonjwa 21 ni raia wa Tanzania, wawili ni raia wa kigeni ,mmoja ni raia wa Ufaransa na mwingine Cuba wote wanaishi Zanzibar.

“Wagonjwa wawili kati ya wagonjwa wapya walifariki nyumbani kabla ya kuchukuliwa vipimo na kufanya jumla ya wagonjwa walifariki kwa maambukizi ya corona kufikia watatu Zanzibar,” alisema Waziri Hamad katika taarifa yake.

Aliwawasisitiza wananchi kuchukua tahadhari zote za kujikinga na ugonjwa huo zinazotolewa mara kwa mara, ikiwamo kuosha mikono kwa maji tirirka na asabuni, kuepuka misongamano na kuahirisha safari za nje na ndani ya nchi zisizo za lazima.

“Wizara inawaomba wananchi ambao wana dalili za homa kali, kukohoa na kupiga chafya kujitokeza katika vituo vyetu vya afya au kupiga simu namba 190 ,ni vema mgonjwa mwenye dalili hizi asijichanganye na wagonjwa au watu wengine na tuache tabia ya kujitibu wenyewe, kwani kufanya hivyo tunaendelea kueneza maambukizi na vifo vitokanavyo na ugonjwa huo,” alisema 

MASHINE ZA ROSTAM 

Katika kuunga mkono juhudi za Serikali za kupambana na virusi vya corona, mfanyabishara maarufu nchini, Rostam Aziz jana alitoa mashine maalumu mbili za kutakasa mwili na mvuke wenye dawa katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili (MNH).

Akizungujmza Dar es Salaam jana, Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano wa MNH, Aminiel Aligaesha alisema uongozi wa hospitali hiyo unamshukuru Rostam kwa msaada huo.

“Mahitaji bado ni mengi, tunaomba wasamaria wema kutusaidia kupata mashine kama hizi 12 ili ziwekwe maeneo mbalimbali ya Hospitali ya Muhimbili,” alisema Aligaesha.

KATIBU MKUU 

Katika hatua nyingine, Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Dk. Zainab Chaula aliishahuri Hospitali ya Taifa ya Muhimbili (MNH), kuendelea kuongeza uzalishaji wa vazi la kujikinga (PPE) kwa ajili ya wataalamu wa afya kujikinga na maambukizi ya virusi vya corona wakati wa kutoa huma kwa wagonjwa. 

Dk Chaula, alisema hayo jana alipotembelea kiwanda kidogo cha kutengeneza mavazi hayo. 

“ Leo (jana), nimekuja hapa kuwatia moyo kwa kazi kubwa mnayoifanya. Sisi kama Serikali tunaichukulia kama jambo jema hasa kipindi hiki cha mapambano ya COVID-19,” alisema Dk.Chaula.

DK. NDUGULILE 

Kutoka na kuwapo mitazamo na mijadala tofauti tofauti kuhusu matumizi sahihi ya barakoa za vitambaa,Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Dk. Faustine Ndugulile, alieleza kuhusu matumizi sahihi ya barakoa.

Kwa mijibu wa Ndugulile barakoa za N95 zinapaswa kutumika na watoa huduma wa afya wanaohudumia wagonjwa wa Covid-19 ambapo barakoa hizo hazipaswi kuvaliwa mitaani, majumbani wala maofisini.

“Barakoa za upasuaji (surgical masks), hizi zinapaswa kuvaliwa na watumishi wa afya ambao hawana direct contact na wagonjwa, pia zinaweza kuvaliwa na jamii kwenye maeneo ya mikusanyiko kwa muda wa saa 4 hadi 6 pia hazipaswi kuvaliwa kutwa nzima na kurudia matumizi (re-use),” alisema 

Alisema kumekuwa na sintofahamu kuhusu namna ya uvaaji wa barakoa za upasuaji ambazo zinatakiwa kuvaliwa kwa usahihi kama njia ya kujinga na maambukizi.

“Upande wenye rangi (blue, kijani, zambarau nk) unapaswa kuwa nje, upande wenye chuma unapaswa kuwa juu.

Akizungumzia kuhusu barakoa za kitambaa nazo zinaweza kutumia ili kupunguza uwezekano wa maambukizi kutoka kwa mtu mmoja kwenda mwingine majumbani na sehemu za mikusanyiko huku akitaka kuzingatiwa kwa kutumia vitambaa vya pamba.

“Kutumia layers zaidi ya mbili katika utengenezaji wa barakoa hizo, kuwa na barakoa angalau mbili ili kuruhusu kufanyiwa usafi wa mara kwa mara, barakoa zifuliwe kwa maji na sabuni na kupigwa pasi,” alisema Dk. Ndugulile.

Alisema matumizi ya barako sio mbadala wa kunawa mikono au kuzingatia umbali kati ya mtu na mtu, bali ni nyongeza za hatua hizo.

“Tuhakikishe barakoa zilizotumika hazitupwi ovyo,badala yale zichomwe moto ili kuepuka kuokotwa na kutumiwa na watu wengine,vile vile watu hawapaswi kuazimana barakoa iliyokwisha kutumika, kila mtu awe na yake na kila mtu aendelee kuzingatia maelekezo yanayotolewa mara kwa mara na Wizara ya Afya kuhusu hatua mbali mbali za kujikinga na ugonjwa huu,” alisema 

TAASISI, MASHIRIKA 

Ili kuhakikisha kuengdelea kuchuka tahadhari taasisi mbalimbali za serikali na binafsi zimeendelea kuhimiza uvaaji wa barako kwa watu wote watakaofika katika maeneo ya Ofisi 

Taarifa iliyotolewa na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), ilielekeza walipakodi na wananchi wote watakaofika katika ofisi hizo kuvaa barakoa 

“Siku ya Jumatatu (leo) na kuendelea wageni wote watakaolazimika kufika ofisi za TRA kote nchini ili kupata huduma mbalimbali, watatakiwa kuvaa barakoa kwa lengo la kujikinga wao wenyewe na wezao na kuzia maabukizi mapya ya virusi vya corona,” alisema 

Mbali na hil,. Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco), liliagiza wateja wake wote wanaofika katika ofisi mbalimbali kuhakikisha wanavaa barakoa kama hatua ya kudhibiti maambukizin ya corona nchini.

Taarifa hiyo, iliyotolewa na Kitengo cha Uhusiano Tanesco, ilieleza hatua hiyo ni kufanikisha maelekezo ya Serikali kwa ufanisi mkubwa.

“Kuanzia Jumatatu (leo), wageni eote watakaofika ofisi za shirika, watalazimika kuvaa barakoa, ndipo wapate ruhusa ya kuingia katika ofisi za shirika, pia kuzingatia taratibu zote za kiusalama zilizowekwa katika ofisi zetu ikiwamo kunawa mikono kwa kutumia vitaksa mikono vilivyowekwa kila ofisi, kabla ya kuingia katika ofisi husika,” ilieleza taarifa hiyo.

WAZIRI UMMY 

Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu, amewataka wananchi waendelee na shughuli zao za uzalishaji na biashara kwa kufuata maelekezo na kuchukua tahadhari ili kujienpusha na maambukizi ya virusi vya corona.

 “Ninawakumbusha wananchi kuepuka misongamano isiyokuwa ya lazima ili kujikinga na maambukizi. Nitumie fursa hii kuwakumbusha Watanzania waendelee kufuata maekezo ya wataalamu wa afya kama kunawa mikono kwa maji tiririka na sabuni na kupuka misongamano,” alisema Ummy katika taarifa yake

MBUNGE ATAKA MWONGOZO

Mbunge wa Viti Maalumu, Upendo Peneza (Chadema) amemuomba Rais Dk. John Magufuli kutoa mwongozo wa kitaifa kuhusiana na ugonjwa wa corona, huku akitaka mkuu wa nchi ndiye awe msemaji mkuu kuhusu hali halisi ya ugonjwa huo.

Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dodoma jana, mbunge huyo alimuomba Rais Magufuli, atoe mwongozo kuhusiana na jinsi ya kukabiliana na ugonjwa huo na hali halisi ilivyo tofauti na sasa ambapo kila mmoja amekuwa akizungumza hivyo kuwachanganya wananchi.

WAKAZI WA DAR

Mkuu wa Wilaya ya Iringa, Richard Kasesera, amewataka wananchi wa wilaya yake kujitenga na abiria wanaofika katika mkoa huo hasa wanaotoka Dar es Salaam kwa kudai huenda wana maambukizi ya corona.

“Tutaendelea kuwamonitor (kuwafuatilia), wanaotoka Dar es Salaa, sitaki kupotesa sura hata moja, wanapoingia tupeni taarifa. Sasa hivi wanaotoka nje ya nchi na anayetoka Dar es Salaam usikae naye karibu hakikisha unatupa taarifa ili tuweze kummonita,” alisema Kasesela.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
587,000SubscribersSubscribe

Latest Articles