Jessca Nangawe
NYOTA wa Bongo fleva, Naseeb Abdul ‘Diamond Platnumz’ akiwa nchini Uingereza amefanikiwa kutwaa tuzo ya Philanthropic Endeavour Community Action Awards kutokana na mchango wake kwenye jamii.
Tuzo hiyo ya heshima imetolewa na kituo cha BOA awards ambacho hutoa tuzo kwa watu maarufu wenye kutoa michango yao kwa jamii zinazo wazunguka.
Diamond ameshinda tuzo hii kutokana na mambo mbalimbali anayoyafanya kuizunguka jamii.
Kupitai kurasa zake za mitandao wa kijamii staa huyo amewashukuru mashabiki zake na kuahidi kuendelea kuwa na ushirikiano baina yake na jamii.
“Nipende kuchukua fursa hii kushukuru kwa mchango wa kila mmoja, tuendeelee kusaidia hasa kwa sisi vijana kuhakikisha tunapamba katika muziki wetu na kutengeneza maisha mazuri kwa kizazi kijacho,” aliandika Diamond.
Mastaa wengine ambao wametwaa tuzo kama hiyo ni pamoja na rapa Fuse ODG wa Uingereza, nyota wa soka wa Crystal Palace, Wilfried Zaha, kiungo wa Chelsea, N’golo Kante.
Lakini kwenye tukio hilo kulikuwa na mastaa mbalimbali kama vile Yaya Toure, Emmanuel Adebayor, Asamoah Gyan Victor Wanyama, Sadio Mane, Alex Iwobi, Andre Ayew na beki wa zamani wa Man United, Rio Ferdinand.