Na BENJAMIN MASESE- BUNDA
WATOTO na mabinti wenye umri kati ya miaka 16 hadi 30 katika Wilaya ya Bunda mkoani Mara wanaongoza kufika katika ofisi za ustawi wa jamii kuomba talaka au kulalamika kutelekezwa na waume zao, imeelezwa.
Pia wakati hali ikiwa hivyo kwa wasichana , takwimu zilizopo Jeshi la Polisi Wilaya ya Bunda zinaonyesha kuwapo na ongezeko kubwa la watoto kufanyiwa ukatili, vipigo na kutelekezwa katika kipindi cha miaka mitatu ya 2016 hadi Juni 2019.
Hayo yalibainishwa na Ofisa Ustawi Wilaya ya Bunda, Fausta Gabriel na Mkuu wa Dawati la Jinsia kutoka Jeshi la Polisi Wilaya ya Bunda, CPL Mbijima Julius katika mikutano ya kampeni ya kupinga ukatili inayotaribiwa na Shirika la Kutetea Wanawake na Watoto la Kivulini.
Akizungumza na wananchi katika mkutano uliohusisha vijiji vya Mihingo, Manchemweru na Mahanga, Fausta alisema katika ofisi yake anapokea malalamiko mengi kutoka kwa watoto na mambinti wenye umri kati ya miaka 16 hadi 30 wakiomba kupewa talaka ili kuachana na waume zao.
Gabriel alisema kwa wiki moja hupokea maombi na malalamiko zaidi ya 15 wakitaka talaka na uchunguzi unaonyesha mabinti waliingia katika mahusiano ya ndoa wakiwa na umri mdogo.
Aliongeza kuwa mabinti wanaofika katika ofisi yake wengi wao wanakuwa na wamejifungua watoto zaidi ya watatu.
“Jamani ni suala la masikitiko kidogo ingawa tunaposema nyinyi mnacheka mnaona ni jambo la kawaida lakini tambueni mnatengeneza kizazi na jamii isiyo na ustawi, uchumi, amani na elimu, mfano kwanza hamna mwamko wa kusomesha watoto wa kike badala yake mnawaandaa kuwaozesha.
“Pale ofisini kwangu napokea malalamiko mengi ya watoto na mabinti ambao waliingia kwenye mahusinao ya ndoa wakiwa wadogo, yaani mwoaji na mwolewaji wote walikuwa watoto sasa inafikia hatua kijana akikuwa kidogo anamkimbia mke wake na kuangalia wengine na kutelekeza familia yake.
“Kwa wiki napokea maombi ya talaka na malalamiko ya kutelekezwa na wanaume zaidi ya 15 hebu fikiria takwimu hiyo kwa mwezi au mwaka inakuaje?, unapotaka kuwakutanisha ili kuwasuluhisha unakuta mume hapatikani, ukiuliza kama wana mali nyumbani unaambiwa hakuna kitu huku tayari mama amezalishwa watoto zaidi ya watatu anatembea nao, hii ni hatari sana,”alisema. Ofisa huyo alisema hata watoto wa kike katika shule za sekondari si wengi ukilinganisha na shule za msingi kwa sababu hawajafikia umri wa kuolewa