LONDON, UINGEREZA
HATIMA ya mchakato wa kujitoa kwa Uingereza kutoka Umoja wa Ulaya maarufu kama Brexit inatarajia kufahamika baadaye wiki hii.
Viongozi wa Umoja wa Ulaya wanasubiri kuona kama matokeo ya mazungumzo kati ya Serikali ya Waziri Mkuu Theresa May na kiongozi wa chama cha upinzani cha Labour yataukwamua mchakato wa Brexit.
Hii inakuja kwa Bunge la Uingereza kutarajia kuupigia kura muswada wa sheria utakaolipatia haki ya kuamua juu ya kurefushwa muda wa kujitoa katika Umoja wa Ulaya.
May anatarajiwa kuwasilisha mapendekezo mapya katika mkutano wa dharura wa viongozi wa Umoja wa Ulaya utakapoitishwa kesho mjini Brussels.
Mkutano huo wa kilele ndio utakaoamua kama mchakato wa Brexit urefushwe au la.