Na Derick Milton
MKOA wa Simiyu umeendelea kutekeleza sera ya Tanzania ya Viwanda baada ya kuanza mchakato wa kuanzisha kiwanda kidogo cha kusindika nyanya kitakachojengwa katika Wilaya ya Busega.
Mbali na kuanzishwa kiwanda hicho, mkoa huo pia umeanzisha mchakato mwingine wa kupanua kiwanda kidogo cha maziwa katika wilaya ya Meatu kuongeza uzalishaji.
Kukamilika kwa viwanda hivyo kutafanya mkoa huo kufikisha viwanda vidogo vitatu kikiwamo Kiwanda Cha Chaki kilichopo wilayani Maswa, kwa kaulimbiu ya ‘wilaya moja kiwanda kimoja’.
Hayo yalibainika katika kikao cha kupokea taarifa ya utafiti wa ujenzi na upanuzi wa viwanda hivyo uliofanywa na shirika la ESRS. Kikao hicho kiliongozwa na Mkuu wa Mkoa, Antony Mtaka.
Akiwasilisha taarifa ya upanuzi wa Kiwanda cha Maziwa Meatu, Profesa Lusato Kurwijila kutoka Chuo Kikuu Cha Kilimo (SUA), alisema ili kuongeza uzalishaji wa kiwanda hicho lazima kuwekeza katika ufugaji wa kisasa.
“Utafiti umeonyesha kuwa wilaya nzima haina kituo hata kimoja cha kukusanyia maziwa, wanatakiwa kwanza kuwekeza katika vituo vya kukusanya maziwa na miundombinu.
“Lakini wanatakiwa Sh bilioni 4.4 kupanua kiwanda hicho,” alisema Profesa Kwilijira.
Naye Geremia Makindala mtaalamu wa kilimo na biashara kutoka SUA akiwasilisha taarifa ya ujenzi wa Kiwanda cha Kusindika Nyanya, alisema utafiti umeonyesha tani 11 za nyanya huaribika kila mwaka katika wilaya hiyo.
“Wakulima wa nyanya wamekuwa wakipata hasara kutokana na kuharibika kwa nyaya zao kwa kukosa soko au kutunza vibaya.
“Ili kiwanda kijengwe lazima wakulima wapewe elimu ya kilimo cha kisasa na kuunda vikundi vya ushirika,” alisema Makindala.
Mkurugenzi wa Wilaya ya Meatu, Fabian Manoza na Mkurugenzi wa Wilaya ya Busega, Andarson Kabuku, walisema utafiti huo umewawezesha kuanza utekelezaji wa ujenzi na upanuzi wa viwanda hivyo.
Mkuu wa mkoa alisema baada ya utafiti huo ni fursa kwa mwekezaji yeyote kufika mkoani humo kujenga na kupanua viwanda hivyo.
“Tunaelekea katika utekelezaji baada ya miaka miwili au mitano Mkoa wa Simiyu kila wilaya itakuwa na kiwanda.
“Hatuwezi kuwa na halmashauri zinazotegemea ushuru wa mama ntilie, tunataka viwanda hivi kuwa vyanzo vya mapato kwenye halmashauri na ajira kwa vijana,” alisema Mtaka.