Na Gabriel Mushi, Dar es Salaam
KAMPUNI ya Simu za Mkononi ya Vodacom Tanzania imesisitiza kuwa itaendelea kuboresha ushirikiano na vyombo vya habari nchini kukuza sekta ya mawasiliano kulingana na mabadiliko ya teknolojia.
Kauli hiyo ilitolewa jana na Mkurugenzi Mtendaji wa Vodacom Tanzania, Ian Ferrao, alipotembelea Kampuni ya Newhabari (2006) Ltd, kufahamu sera na mipango ya kampuni hiyo katika mabadiliko ya teknolojia nchini.
Alisema Watanzania wamekuwa na mwamko mkubwa wa matumizi ya simu za mikononi hivyo ni vema sekta ya habari ikabadilika na kuanzisha huduma za kupata habari kwa njia ya simu kuongeza mapato.
“Ni wakati sasa wa kujiunga na application mbalimbali kama M-paper na nyingine kurahisisha magazeti yenu kusomwa zaidi na wananchi, bila kusahau ile huduma ya ‘breaking news’ ambayo imekua kwa kasi kutokana na wananchi wengi kuwa na simu zenye huduma za internet,” alisema.
Hata hivyo alisema Vodacom itaendelea kufadhili mafunzo mbalimbali ya waandishi wa habari kuongeza uelewa wao kuhusu mambo mengi hususan katika sekta ya biashara na kodi.
“Tumekuwa tukifadhili mafunzo ya waandishi wa habari kupitia vyama vyao kama vile Chama cha Waandishi wa Habari za Kodi (TAWNET) lakini hatutoishia hapo, tutaendelea kuwaunga mkono i watakapokuja kuhitaji msaada zaidi.
“Tunafurahi kuona mchango wa Vodacom katika kuleta maendeleo nchini na kubadilisha maisha ya Watanzania kuwa bora, hivi sasa tumejizatiti kuboresha huduma za mawasiliano nchini na tutaendelea kubuni huduma mbalimbali za kutumia teknolojia ya simu kurahisisha maisha ya wananchi.
“Vodacom imejizatiti kuboresha huduma zake, taasisi yake ya kuboresha huduma za jamii ya Vodacom Foundation imejikita kuendelea kutoa misaada mbalimbali kwa jamii,” alisema.
Naye Ofisa Mtendaji Mkuu wa kampuni ya Newhabari, Husein Bashe, alitoa wito kwa kampuni hiyo kuendelea kubuni huduma zitakazowafikia watu wengi zaidi vijijini.
“Vijijini kunakuwa na siku za magulio kwa mfano kama Nzega, kwa wiki kuna siku tatu za magulio, hivyo mnaweza kuwapata wateja wengi wa huduma zenu na kuongeza mapato.
“Lakini pia kuhusu suala la breaking news, hili tumeshaandaa mkakati wa kulitekeleza na tutahitaji ushirikiano nanyi zaidi kuona namna ya kuboresha huduma hii kati ya kampuni hizi mbili,” alisema.
Mhariri Mtendaji Mkuu wa kampuni hiyo, Absalom Kibanda, aliitaka Vodacom kuzingatia siku za mwisho wa wiki katika utoaji wa matangazo yao kwa vile ni siku ambazo wananchi wengi huwa wametulia majumbani kwao na kuweza kusoma magazeti kwa umakini.
“Siku kama za Jumamosi na Jumapili, hizi si siku za kudharau kwa sababu tunaona mnakimbilia zaidi siku za wiki mkidhani mtapata wasomaji wengi wa matangazo yenu, la hasha!
“Siku hizi zina umuhimu wa pekee kwa sababu wasomaji wengi wametulia majumbani mwao,” alisema.
Kibanda pia aliitaka kampuni hiyo kuzingatia aina ya matangazo na magazeti inayoyalenga.
“Inashangaza kuona Vodacom wadhamini wakuu wa Ligi Kuu ya mpira wa soka nchini lakini cha ajabu hamtangazi kwa kina katika magazeti ya michezo.
“Wakati umefika sasa wa kubuni miradi ili kulenga wasomaji pia wa michezo na kuongeza mapato,” alisema.