23.4 C
Dar es Salaam
Saturday, April 27, 2024

Contact us: [email protected]

Mbunge aliyepata ajali atakiwa kupumzika

Na VERONICA ROMWALD -DAR ES SALAAM

JOPO la madaktari wa Taasisi ya Mifupa Muhimbili (MOI), linalomuhudumia Mbunge wa Viti Maalum Mkoa wa Dodoma, Kunti Yusuf Majala (Chadema), aliyejeruhiwa katika ajali ya gari, limempa muda wa kupumzika.

Ofisa Uhusiano wa MOI, Patrick Mvungi alisema hayo jana alipozungumza na MTANZANIA lilipohitaji kumtembelea wodini mbunge huyo.

“Madaktari wanaomuhudumia wameshauri apumzike, wamempa muda, hivyo sasa hawezi kufanya mahojiano na chombo chochote cha habari,” alisema Mvungi.

Alisema pamoja na hayo hali ya mbunge huyo na majeruhi wengine imeimarika.

“Nimetoka muda si mrefu kumuona wodini, wote wanaendelea vizuri, hawajambo,” alisema.

Mbunge huyo amelazwa MOI kwa matibabu zaidi baada ya kupata ajali akiwa na familia yake mkoani Dodoma.

Alisafirishwa kwa ndege juzi pamoja na majeruhi wengine akitokea Hospitali ya Mkoa wa Dodoma na kufikishwa Hospitali ya Taifa Muhimbili kisha kuhamishiwa MOI.

Taarifa iliyotolewa jana na Idara ya Habari na Mawasiliano ya Chadema ilieleza kuwa mbunge huyo na familia yake walisafirishwa kuja Dar es Salaam kwa matibabu zaidi kutokana na hali zao baada ya kupata ajali hiyo.

“Hadi sasa watu wawili wa familia yake wamethibitishwa kufariki kutokana na ajali hiyo iliyotokea eneo la Nchemba, wakati Kunti pamoja na familia yake walipokuwa wakielekea Kondoa, mkoani Dodoma kwa shughuli ya kifamilia,” ilielezwa.

Ilielezwa kulingana na taarifa za awali, hadi sasa mbali ya mbunge huyo, majeruhi wengine ni pamoja na dereva wa gari hilo lililopata ajali, Stephen Massawe ambaye pia ni dereva wa Chadema Kanda ya Kati na watu wengine sita, wote ni wa familia yake.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles