25.2 C
Dar es Salaam
Friday, April 26, 2024

Contact us: [email protected]

‘WANAWAKE WENGI WANAAMINI NI HALALI KUPIGWA NA WAUME ZAO’

 

Na JUDITH NYANGE


ASILIMIA 58 ya wanawake wilayani Misungwi  wanaamini ni halali kupigwa na waume zao endapo watashindwa kutekeleza masuala mbalimbali ikiwamo kuunguza mboga.

Hayo yalielezwa juzi na Mkurugenzi wa Shirika la Kutetea Haki za Wanawake Kivulini, Yassin Ally wakati wa uzinduzi wa awamu ya pili ya programu ya kutokomeza ukatili wa  jinsia dhidi ya wanawake na wasichana (GBVII).

Alisema   walipoanza programu  ya GBVI katika kata tano,  waligundua   kiwango cha ukatili  katika Wilaya ya Misungwi  kilikuwa asilimia 56 lakini baada ya utekelezaji kilishuka na kufikia asilimia 36.

“Kwa mujibu wa tathimini ya  taifa ya mwaka 2015/16,  asilimia 58 ya wanawake wilayani Misungwi wanasema ni halali kwa mwanaume kumpiga endapo  ameunguza mboga, kuondoka bila kuaga na kutotunza watoto hata kama hajapatiwa  matumizi,” alisema Ally.

Alisema pia katika  Wilaya ya Misungwi ilibainika wananchi wengi wananyamaza wanapofanyiwa ukatili.

Hata hivyo alisema   baada ya utekelezaji wa GBVI wameweza kufichua matukio mbalimbali  likiwamo la   polisi  aliyebaka na kuhukumiwa kifungo cha miaka 30.

Naye Waziri wa Mambo ya Nje wa Ireland, Ciaran Cannon, alisema  ukatili wa  jinsia uwe wa  mwili, ubakaji, kujamiana,  hisia au  uchumi  unatambulika uduniani kote na  unajulikana kama moja ya ukiukwaji wa haki za wanawake na wasichana.

“Nchini Ireland ukatili wa majumbani  ni tatizo, mwanamke mmoja kati ya saba ameathirika na ukatili wa  mwili,  ihisia au  uchumi kutoka kwa mwenza wake katika maisha yake.

“Kwa Tanzania asilimia 40 ya wanawake wamekumbwa  na ukatili  wa  mwili na mwanamke mmoja kati ya watano ameshapitia unyanyaswaji  katika maisha yake,” alisema Cannon.

Alisema tatizo la unyanyasaji linasababisha  gharama kubwa kwa  kwa jamii, familia na nchi kwa ujumla pamoja na upatikanaji wa kipato.

Alisema  ndiyo sababu serikali ya nchi yake kupitia Mfuko wa Maendeleo wa Ireland  imetoa fedha kwa Shirika la Kivulini kwa ajili ya kupinga ukatili wa  jinsia.

Mkuu wa Mkoa wa Mwanza, John Mongella, alisema unyanyasaji wa  jinsia  ni jambo lililopitwa na wakati  katika zama hizi na  wote wanaoshiriki kuliendeleza ni washamba .

“Kwenye jamii zetu bado kuna unyayasaji lakini hili ni jambo lilitopitwa na wakati sana, kama kuna mtu bado anashiriki unyanyasaji wa watoto, wanawake na kama kuna mama anashiriki unyanyasaji wa kina baba ajijue yeye ni mshamba na amepitwa na wakati.

“Hakutakiwi kuwe na mama anayemnyanyasa baba wala baba anayemnyanyasa mama wala mtu anayenyanyasa watoto, awe wa kiume au wa kike, hatutegemei mambo haya yaendelee,” alisema Mongella.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles