23.6 C
Dar es Salaam
Friday, April 26, 2024

Contact us: [email protected]

Serikali kukuza ujuzi uzalishaji ajira nchini

Na MWANDISHI WETU-ARUSHA

SERIKALI imeendelea kuongeza ubora wa elimu na kukuza ujuzi ili kuongeza tija katika uzalishaji na kuongeza ajira nchini.

Hatua hiyo imekuja baada ya kuwekwa kwa sera, mifumo na miundombinu wezeshi kwa Watanzania kuweza kupata ujuzi na umahiri unaohitajika katika kuiwezesha Tanzania kufikia malengo ya mpango wa maendeleo 2025 na malengo endelevu ya milenia.

Kauli hiyo imetolewa mwishoni mwa wiki jijini Arusha na Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa Joyce Ndalichako, akifungua mkutano mkuu wa tatu wa kimataifa wa nishati endelevu na teknolojia ya maji 2019.

Profesa Ndalichako alisema lengo la mkutano huo ni kujadili changamoto zinazokabili sekta ya nishati, hususan kukuza nishati mbadala na teknolojia ya miundombinu ya maji.

Alisema lengo la Serikali ni kuhakikisha elimu itolewayo inakuwa bora na kuendeleza ujuzi kwa Watanzania ili waweze kuongeza thamani katika mazao kutumia teknolojia ya kisasa, na kwamba maji na nishati ni maeneo muhimu katika kutekeleza hili.

“Tunataka kuona kama ni mkulima anakuwa na uwezo wa kuongeza thamani ya mazao kwa kutumia teknolojia za kisasa na hasa kutumia tafiti zilizofanywa,” alisema.

 Profesa Ndalichako aliipongeza Taasisi ya Sayansi na Teknolojia ya Nelson Mandela (NM-AIST) kwa kuboresha kiwango cha utafiti katika chuo hicho ikiwa ni pamoja na programu wanazotoa.

“Mwaka 2017 hapa NM-AIST tumefanya uzinduzi wa vituo vinne vya umahiri vya sayansi na teknolojia katika elimu ya juu kwa lengo la kuhakikisha tunaboresha elimu yetu na kunakuwa na wigo mpana wa kufanya tafiti.

“Tunaona sasa mnafanya vizuri na kuendana na moto wa chuo ambao ni ‘Taaluma kwa jamii na viwanda’, na hata maji ya kunywa yanayotumika katika mkutano huu ni moja ya kazi za tafiti zinazofanyika hapa,” alisema.

Makamu Mkuu wa NM-AIST ambaye pia ni Mwenyekiti mwenza wa ICEAS, Profesa Emmanuel Luoga, alisema mkutano huo umewaleta pamoja wataalamu wa nishati mbadala na endelevu na watafiti kutoka nchi mbalimbali.

Alisema mada 37 zitawasilishwa na wataalamu kutoka nchi 11 zilizoshiriki mkutano huo.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles