24.8 C
Dar es Salaam
Friday, April 26, 2024

Contact us: [email protected]

SEKTA YA VIWANDA YAIMARIKA ZANZIBAR

ZANZIBAR iko katika hatua za mwisho  za utengenezaji wa Sera ya Viwanda ili kuwezesha ukuaji wa Sekta hiyo kufuatia mahitaji yake ambayo kukosekana kwake kumesababisha ukuaji mdogo  wa  uwekezaji ukifananisha na kile kinachofanyika bara ambako kumeshamiri.

Sera ya viwanda mara nyingi hutambua mahitaji halisi ya nchi husika na kuweka vigezo stahiki vya uwekezaji vikiambatana na utoaji mwafaka wa vivutio kwa kwa wawekezaji wanaounga mkono  sera hiyo kama ilivyoainishwa.

Wizara ya Biashara, Viwanda na Masoko  ya          Zanzibar imesema sekta ya viwanda inazidi kuimarika katika thamani ya uzalishaji viwandani kutoka Shilingi  bilioni 4.17 hadi kufikia Shilingi  bilioni 4.87 kwa mwaka jana ikiwa ni ukuaji wa asilimia  12.

 

Balozi Amina Salum Ali  ambaye ni Waziri wa Biashara, Viwanda na Masoko alisema hayo wakati akitoa maelezo mbele ya Rais wa Zanzibar, Dk Ali Mohamed Shein, Ikulu mjini Unguja na kubainisha hatua waliyofikia kwa  kuelezea hatua iliyofikiwa ya sera ya Viwanda na kutoa umuhimu wake kwa  sekta binafsi  na kuipongeza kwa mchango wake  chanya.

“Tupo katika hatua za mwisho za mchakato wa kukamilisha sera ya viwanda itakayokuwa mwongozo katika kuimarisha sekta hiyo na kuchangia pato la taifa…, lakini tunaipongeza sekta binafsi kwa kuitikia wito wa uwekezaji wa viwanda,” alisema Balozi Amina.

Kabla ya maelezo hayo Dk Shein alifurahishwa na mazingira yaliyooneshwa ya wawekezaji  kuchangamkia kuwekeza katika sekta za viwanda huku akisisitiza kwamba  Serikali yake imeimarisha mazingira ya uwekezaji  na ikikamilika sera  itakuwa kivutio kwa wawekezaji wengi

Alizitaka taasisi za uwekezaji  Zanzibar ikiwemo Mamlaka ya Vitega Uchumi (ZIPA) kujenga mazingira mazuri yatakayowafanya wawekezaji kuja kuwekeza katika miradi mbalimbali ya maendeleo.

Ripoti zilizopo zinaonesha  kuwa  uwekezaji huo umeimarika   zaidi katika viwanda vya kazi za ujenzi ikiwemo kusaga kokoto pamoja na matofali.

Waziri huo alisema uwekezaji katika Kampuni ya Azam umeongeza uzalishaji wa bidhaa za maziwa na hivyo kuongeza ajira.

Alivitaja viwanda vingine vilivyoimarisha uzalishaji na ajira kuwa ni pamoja ni viwanda vya maji ya chupa.

Wakati huo huo habari toka Pemba zinaonesha  kuwa shughuli ya  kutafuta mafuta imeanza visiwani humo.

 

Utafutaji mafuta

 

Kazi za utafiti wa nishati ya mafuta kwa kutumia meli zinatarajiwa kuanza katika ukanda wa Kisiwa cha Pemba kwa mujibu wa taarifa ya Makamu wa Pili wa Rais, Balozi Seif Ali Iddi  amabaye amezindua utafutaji wa nishati ya mafuta kwa kutumia meli baharini leo.

Mtaalamu wa mafuta kutoka Kampuni ya Rakgas ya Rasilkhema, Sharif Hassan alisema kazi za utafiti zitafanywa na Kampuni ya BGP kutoka China kwa kutumia meli katika ukanda wa bahari ya Pemba na Unguja.

Akifafanua, alisema kazi za utafiti wa mafuta kwa njia ya bahari zimezingatia athari zote za mazingira ikiwemo kwa wavuvi na viumbe vya baharini ili wasipate  matatizo yanayoweza kuzuilika

Katibu Mkuu wa Wizara ya Maji, Nishati, Ardhi na Mazingira, Ali Halil Mirza alisema hatua iliyofikiwa sasa ni kufanya utafiti kujua kama nishati ya mafuta ipo au hakuna.

“Tumezingatia masuala ya athari za mazingira kwa viumbe wa baharini ambapo kabla ya kufanya kazi hiyo, utafiti zaidi utafanyika kujua aina ya samaki waliopo baharini  na rasilimali nyinginezo  zitakazoweza kuvunwa kikamilifu, ” alisema Hassan wa  BGP.

Mirza alisema utafiti uliofanyika katika hatua za kwanza ulikuwa wa kupigapicha ardhini kwa kutumia ndege ambayo matokeo yake yanafanyiwa  uchambuzi  na yanatazamiwa kujulikana  kwa ukamilifu  wake hivi karibuni.

Hassan alibainisha kuwa kazi zinazofanyika kwa sasa ni utafiti wa mafuta uliofanyika kwa njia ya kupiga picha kwa kutumia ndege ardhini .

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles