23.6 C
Dar es Salaam
Saturday, April 27, 2024

Contact us: [email protected]

Mfanyabiashara wa madini Arusha afariki dunia

ELIYA MBONEA-ARUSHA

Mwili wa mfanyabiashara na mmiliki wa migodi ya madini ya vito ya Tanzanite iliyopo Mirerani wilayani Simanjiro mkoani Manyara Thomas Mollel aliyefariki akiwa Dodoma utarajiwa kusafirishwa kesho kwenda mkoani Arusha.

Mollel aliyekuwa Diwani wa Kata ya Mbuguni (CCM) na Mjumbe wa Kamati ya Siasa ya CCM wilaya ya Meru mkoani alisafiri kwenda Bungeni mjini Dodoma kuhudhuria kuapishwa kwa Mbunge mpya wa Jimbo la Arumeru Mashariki John Pallangyo.

Marehemu Mollel atakumbukwa kwa tukio kubwa la kupata madini ya Tanzanite aliyouza kisha kupata fedha nyingi zilizomfanya kupanda juu ya ghorofa la Hoteli yake ya Pallson mjini Arusha kisha kumwaga fedha chini na watu kuanza kuokota.

Akizunguzamza na Mtanzania Digital akiwa mjini Dodoma, Katibu Mwezi wa CCM Mkoa wa Arusha Shaban Mdoe amesema, marehemu aliwasili mjini humo Jumatatu Mei 20, Saa 3 usiku akitokea mkoani Arusha.

“Alipofika mjini alitupigia simu akiuliza tuko wapi kwa vile ulikuwa ni muda wa kupata chakula cha usiku tulimwelekeza kwamba tupo mgahawa wa Rose Garden ambapo alikuja tukapata chakula pamoja.

“Akiwa pale hakuonyesha kama mtu mwenye tatizo kwani alikuwa mchangamfu na mwenye furaha Saa 4 usiku tuliondoka kila akielekea alipofikia yeye alikwenda kupumzika kwa ajili ya kukutana Jumanne,” alisema Mdoe.

Ameendelea kubainisha kwamba ilipofika Saa 5 usiku alipigiwa simu akijulishwa kwamba Mollel ameanguka hivyo anapelekwa Hospitali ya Mkoa wa Dodoma kwa ajili ya uchunguzi zaidi wa afya yake.

“Ndani ya dakika 20 tukiwa tunajiandaa kwenda tulipokea simu nyingine tena ikitujulisha kwamba Mollel amefariki,” amesema Mdoe.

Alipouliza kuhusu taratibu za kusafirisha mwili wa marehemu Mollel Mdoe amesema taarifa rasmi hazijatolewa lakini wanatarajia mara baada ya kuapishwa kwa Mbunge mteule Pallangyo wataanza shughuli ya kuusafirisha mwili huo kuelekea Arusha.

“Kwa hakika tumepoteza mtu muhimu kwa CCM kwani alikuwa muhimili mkubwa kwa Chama kutokana na uwezo wake  wa kiuchumi na ushawishi aliokuwa nao,” amesema Mdoe.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles