24.2 C
Dar es Salaam
Friday, April 26, 2024

Contact us: [email protected]

Maximo awapa mbinu mpya wachezaji

Marcio Maximo
Kocha wa Yanga, Marcio Maximo

NA MWALI IBRAHIM, DAR ES SALAAM

KOCHA wa Yanga, Mbrazil Marcio Maximo, ameanza kuwapa mbinu mpya washambuliaji wake, Said Bahanuzi, Jerry Tegete, Hussein Javu na Nizar Khalfan pamoja na mabeki, ili kujiweka sawa kwa msimu ujao wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara (VPL) na michuano ya Kombe la Shirikisho Afrika.

Yanga jana asubuhi ilihamia kwenye Uwanja wa Shule ya Sekondari Loyola, ikitokea Uwanja wa Bandari uliopo Tandika ilipokuwa ikifanyia mazoezi yake ya awali na leo asubuhi itaingia katika mazoezi ya viungo kwenye gym ya klabu ya Gymkhana, jijini Dar es Salaam.

Katika mazoezi hayo, Maximo aliwafundisha mbinu tatu wachezaji wake ambazo alikuwa akizitumia wakati alipokuwa akikinoa kikosi cha Taifa ‘Taifa Stars’ miaka minne iliyopita, zikiwa ni kucheza kwa kulinda goli zaidi na kufunga mabao kutumia krosi pamoja na kupiga pasi fupi.

Maximo pia aliwafundisha washambuliaji hao kufunga mabao kwa kutumia mashambulizi ya pembeni mwa uwanja kupitia winga wa kushoto na kulia, walikuwa wakipokea pasi kutoka kwa viungo wa kati na mabeki wa pembeni waliokuwa na kazi ya kuwapa mipira mawinga wao kwa ajili ya kupiga krosi za mabao.

Aliwafundisha mabeki wa kati jinsi ya kuzuia mabao yatokanayo na krosi za timu pinzani watakazokutana nazo, aliwagawa wachezaji katika makundi tofauti tofauti kwa ajili ya kujifunza mbinu hizo.

Mazoezi hayo pia yalihudhuriwa na wachezaji wengi wa kikosi cha pili, wote walianza kwa kufanya mazoezi ya viungo na baadaye kufanya mazoezi rasmi ya uwanjani.

Maximo aliyeanza kuifundisha Yanga Jumanne, akirithi mikoba ya Mholanzi Hans Van De Pluilm, ameonekana kuwa mwarobaini wa timu hiyo kutokana na mashabiki kuwa na imani naye.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles