24.1 C
Dar es Salaam
Friday, April 26, 2024

Contact us: [email protected]

Kardinali Pell ashindwa rufaa tuhuma za ngono kwa watoto

MELBOURNE, AUSTRALIA

KARDINALI wa Kanisa Katoliki, George Pell jana alirejeshwa gerezani baada ya mahakama ya Australia kutupa rufaa yake dhidi ya hatia ya dhuluma za kingono dhidi ya watoto.

Alitiwa hatiani kwa kuwabaka wavulana wawili miaka ya 1990.

Pell ataendelea kutumikia kifungo chake cha miaka sita kwa kuwashambulia kingono wavulana wawili wenye umri wa miaka 13 waliokuwa wanaimba kwaya kwenye kanisa mjini Melbourne miaka ya 1990.

Pell mwenye umri wa miaka 78 alikuwa amevaa suti nyeusi na mara kwa mara alikuwa akiinamisha kichwa chake wakati Jaji Mkuu Anne Ferguson akisoma hukumu yake huku kundi la watu lililokusanyika nje ya mahakama hiyo likishangilia.

Jaji Ferguson alisema Pell atastahili kupewa msamaha baada ya miaka mitatu na miezi minane, ingawa Kardinali huyo anaweza bado kuiomba mahakama ya juu ya Australia kusikiliza rufaa zaidi.

Pell ndiye kiongozi wa juu zaidi wa Kikatoliki kutiwa hatiani kwa makosa ya udhalilishaji wa watoto kingono, na kuifanya kesi yake pamoja na hukumu ya jana kuwa  uthibitisho kwa waumini na makundi ya wahanga kote duniani.

Kardinali Pell alisaidia huko nyuma kuwachagua mapapa, alisimamia hazina ya Vatican na alishiriki katika uitikiaji wa Kanisa la Australia juu ya madai ya udhalilishaji wa kingono dhidi ya watoto.

Mawakili wa Pell waliainisha vipingamizi 13 dhidi ya hatia zake, na kutilia shaka kila kitu kuanzia uwezekano wa kimwili wa Pell kuvua majojo yake kumbaka mvulana, hadi kwenye uaminifu wa shahidi mkuu.

Kesi hiyo haikuwa ya kawaida kwa sababu ilitegemea zaidi ushahidi wa mhanga pekee aliesalia hai.

Wawili kati ya majaji wamemwelezea mhanga kama shahidi mwenye heshima ambaye hakuwa muongo, asie na njozi na shahidi wa ukweli.

Mmoja wa wahanga wa Pell alitoa maoni yake katika taarifa iliyosomwa na wakili wake, Vivian Waller, baada ya hukumu ya mahakama dhidi ya rufaa ya Pell.

“Nimetulizwa na uamuzi wa mahakama ya rufaa. Ni miaka minne sasa tangu niliporipoti polisi. Mchakato wa jinai unachosha.

“ Safari hiyo imenipeleka maeneo mengi, ambayo nilihofia kwamba nisingeweza kurejea. Lakini nashukuru kwamba mahakama imempa Pell fursa ya kupinga mashtaka, na kila fursa ya kusikilizwa. Natumai tu kwamba sasa yote yameisha.”

Wakili wa baba wa mtoto wa pili ambaye alifariki kutokana na kubugia dawa mwaka 2014 amesema alihisi kuondolewa mzigo mzito mabegani kwake.

Waziri Mkuu wa Australia Scott Morrison ameelezea huruma kwa wahanga hao, na kusema mahakama imefanya kazi yake, na amesema Kardinali Pell atanyang’anywa nishati yake ya heshima baada ya kushindwa rufaa yake.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles