25.2 C
Dar es Salaam
Friday, April 26, 2024

Contact us: [email protected]

BOBBI-JO WESTLEY: NATAKA NIVUNJE REKODI YA MAPAJA MAKUBWA DUNIANI

NA JOSEPH HIZA NA MASHIRIKA

ANA uzito wa 38 stone sawa na kilo 241 lakini ameapa kuendelea kuuongeza hadi atakapotimiza ndoto yake-kuvunja rekodi ya dunia ya kuwa na mapaja makubwa zaidi duniani.

Mwanamke huyu mkazi wa York, Pennsylvania nchini Marekani, Bobbi-Jo Westley tayari ana mapaja ya inchi 95, lakini amelenga yaongezeke kufikia inchi 99.

Lengo ni kuivunja rekodi iliyowekwa na mkazi wa Los Angeles, Mikel Ruffinelli licha ya kufahamu kuwa hilo linaweza kugharimu maisha yake.

Ukubwa wa mapaja ya mwanamama huyo mwenye umri wa miaka 42 tayari umempatia mashabiki wengi duniani, ambao hununua na kufanya biashara kupitia picha zake duniani.

Bobbi, ambaye anaishi na mumewe alisema: “Mapaja yangu hunifanya niwe wa kipekee. Yananifanya niwe mimi  kama mimi.

“Wakati nilipobaini kuna wanaume wanaopenda umbo langu, nilishangaa sana.

“Napata kila aina ya zawadi na ujumbe kutoka kwa mashabiki wangu, baadhi huniuliza ‘upo tayari kuolewa nami?’ kitu ambacho ni kigumu kwa vile tayari nina mume.”

Si mitizamo yote anayopata Bobbo-Jo mwenye urefu wa futi 5 na inchi 2 mtandaoni inayofurahisha, lakini hupuuza kauli za kuchukiza zinazoibuka kuhusu umbo lake hilo.

Anasema: “Wakati ninapokutana na watu katika mitandao ya jamii wakisema mimi ni mnene, kwa kweli siitikii. Kwa sababu mimi ni mnene na hilo li wazi.”

Lakini wakati umbo lake kubwa likiingiza pesa, limemuathiri kimwili na kumfanya awe chini ya maelekezo ya daktari.

Huhangaika kukamilisha shughuli za msingi za kila siku kwa vile hupata shida kupumua kwa kutembea tu chumbani.

Anasema: “Mara ya mwisho nilipoonana na daktari nilikuwa na uzito wa 542 lbs sawa na kilo 245.8.

“Kwa kweli kuwa na mapaja makubwa si kitu rahisi. Wakati ninapopanda na kushuka ngazi au kupita milangoni, inabidi nipite upande upande.”

Bobbi-Jo anahusisha uzito wake huo mkubwa na maradhi ya tezi dundumio, hali ambayo alikutwa nao wakati akiwa na umri wa miaka sita.

Kwa kazi tezi hiyo ina kazi kubwa ya kuzalisha homoni, kinyume chake hutokea athari ikiwamo ongezeko kubwa la uzito.

Hata hivyo, hivi karibuni alitembelewa na mtaalamu wa mlo na virutubishi Nadia Sharifi, ambaye anamiliki vituo vya upunguzaji uzito na ustawi wa afya ya mwili vya MyTrimLine, ambaye hakukubaliana na maelezo ya Bobbi-Jo.

Nadia alihitimisha kwamba Bobbi-Jo ni ‘bomu linalosubiri kulipuka’, akisema anahitaji kuanza ulaji sahihi au akumbane na kifo cha mapema.

Mtaalamu huo wa mlo alisema: “Ni uchaguzi wa maisha au kifo anaotakiwa auchukue kwa sasa.

“Homoni au masuala ya dundumio, au aina ya damu au urithi vinaweza kutoa mchango mdogo tu wa unene wake bali mchawi mkubwa ni kile anachoingiza katika mdomo wake,” Nadia alisema.

“Wakati tunapozungumzia kuhusu mishipa yake ya damu, inaweza kuziba kirahisi. Kwa kweli ni bomu linalosubiri kulipuka.

“Yuko mahali ambapo hakika ni vigumu kwa watu kupafikia– si kwamba anahitaji kupunguza uzito wa pauni 50 sawa na kilo 22.8 bali pauni zaidi ya 200 sawa na zaidi kilo 90,” anaonya.

Pamoja na maneno hayo ya onyo, Bobbi-Jo anasema harudi nyuma kwa kile moyo umepanga.

Anataka kuwa mmiliki wa mapaja makubwa zaidi duniani, na kwamba hana mpango wa kupunguza uzito hadi atakapotimiza ndoto yake.

Anasema: “Nafahamu kuwa najiweka katika hatari kwa kujaribu kupata mapaja makubwa kabisa duniani.

“Wakati mwingine ni kweli huwa na wasiwasi na afya yangu kwa sababu ya ukubwa – nafahamu fika huu si uzuri wa afya.”

Lakini hakuna ninachopenda bila kujali litakalotokea kama kuweka kumbukumbu hii duniani;-mtu akiuliza ni ‘nani mwenye mapaja makubwa zaidi duniani,’ jibu liwe Bobbi-Jo Westley’!.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles