25.2 C
Dar es Salaam
Friday, April 26, 2024

Contact us: [email protected]

Nyumba 388 Kinondoni kuvunjwa kupisha mradi

mhoweraNA TUNU NASSOR, DAR ES SALAAM

NYUMBA 388 katika Manispaa ya Kinondoni jijini Dar es Salaam, zinatarajiwa kuvunjwa kupisha mradi wa kuboresha kingo za Mto  Ng’ombe utakaoanza kujengwa hivi karibuni.

Akizungumza na MTANZANIA Dar es Salaam jana, Ofisa Uhusiano wa Manispaa ya Kinondoni, Sebastian Mhowera, alisema Sh bilioni 4.4 zinahitajika kwa ajili ya kulipa fidia kwa wakazi wa maeneo hayo.

Alisema ujenzi wa mradi huo utaanzia Ubungo Msewe kupitia Bonde la Mkwajuni na kuishia Daraja la Salenda.

“Tayari tumeanza kuzitambua na kuzitathmini nyumba zote zitakazovunjwa kwa kuziwekea alama ya X. Zinahitajika Sh bilioni 4.4 tuwalipe fidia wananchi ndipo wafadhili wetu watoe fedha za mradi,” alisema Mhowera.

Alisema kata nane za manispaa hiyo zitapitiwa na mradi huo ambazo ni Ubungo, Sinza, Tandale, Manzese, Kijitonyama, Hananasif, Magomeni na Mwananyamala.

Kwa mujibu wa Mhowera, mradi huo utagharimu Dola za Marekani milioni 300 ambazo ni sawa na Sh bilioni 660 ambazo zitatumika katika uboreshaji huo.

Mhowera alisema mbali ya kuboresha mto huo, fedha hizo zilizotolewa na Benki ya Dunia (WB) kama msaada pia zitaboresha miundombinu ya jiji la Dar es Salaam kama barabara, madaraja, mifereji ya maji taka na uzoaji taka.

Wakati huo huo manispaa hiyo imeendelea kuweka alama ya X katika nyumba zilizojengwa katika hifadhi za barabara, maeneo ya wazi na mengine yaliyotengwa kwa ajili ya huduma za kijamii kulingana na mpango mkuu.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles