PATRICIA KIMELEMETA-DAR ES SALAAM
SHAHIDI wa pili katika kesi ya uchochezi inayowakabili viongozi tisa wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo(Chadema), Shaban Abdallah (19), ameieleza Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu kuwa alimuona Mwenyekiti wa chama hicho, Freeman Mbowe, akiwahamasisha wananchi kuendelea kuandamana huku akiwasogelea polisi licha ya tangazo la kuwataka kutawanyika kutolewa na askari hao.
Shahidi huyo ambaye ni mchomelea vyuma na mkazi wa Kinondoni Moscow, alieleza hayo jana mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu Thomas Simba, wakati akiendelea na ushahidi wa upande wa Jamhuri.
Akiongozwa na wakili wa Serikali Mkuu, Paul Kadushi, shahidi Abdallah alieleza kuwa, Februari 16, 2018 asubuhi alikuwa katika eneo lake la kazi eneo la Kinondoni Moscow ambako huwa anafanya kazi ya kutengeneza vitanda na vyuma.
Alisema ilipofika saa 11 jioni alipewa fedha na bosi wake kwenda eneo la Mkwajuni kununua vifaa vya kazi na alifika dukani kwa mtu aliyemtaja kwa jina la Baba John na kununua vitu hivyo.
“Wakati tulipokua tukifanya hesabu na baba John na kabla ya kuchukua mzigo, kwa mbali nilisikia zogo, lakini sikuzifuatilia sana.
“Lilipozidi kusogea ndipo tulipoamua kutoka dukani na Baba John na kwenda nje kuangalia ambako tuliona watu wengi katikati ya barabara wakitokea eneo la Morocco na kuelekea eneo la Magomeni huku wakiwa wameshika mawe na marungu,” alieleza Abdallah.
Alisema waandamaji hao walionekana kuwa katika hali ya shari na walikuwa wakiimba ‘Hatupoi mpaka mmoja afe, watatuua’ kwa kuwaangalia yeye na Baba John walijua kuwa ni watu wa Chadema kwa kuwa walikuwa wamevaa fulana za Chadema, skafu na bendera huku viongozi wao wakiwa mbele.
Alieleza kuwa viongozi hao aliyowatambua ni pamoja na Mbowe, Mdee, Mnyika na Matiko ambao wote ni washtakiwa katika kesi hiyo.
Shahidi huyo wa pili aliieleza Mahakama kuwa wakati wakiendelea kuwaangalia waandamanaji hao waliona gari la polisi likija nyuma yao huku likiwatangazia watawanyike lakini waliendelea kuandamana na kulisogelea gari hilo na kuanza kuwarushia chupa za maji, mawe na marungu.
Alieleza kuwa alipoangalia alimuona Mbowe akiwahamasisha wananchi kuendelea kuandamana na kuwasogelea askari huku wakiwa na viongozi wengine.
Abdallah alieleza kuwa baada ya hapo, askari walianza kupiga mabomu ya machozi na kila mtu alikimbilia njia yake.