25.2 C
Dar es Salaam
Friday, April 26, 2024

Contact us: [email protected]

Wafungwa waliosamehewa na Rais Samia wauawa kwa wizi

Na Gustafu Haule,Pwani

Wafungwa wawili waliosamehewa April 12, mwaka huu na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Samia Suluhu Hassan wameuawa na wananchi wenye hasira kali baada ya kukutwa wakiiba huko katika eneo la kwa Mathias Kibaha.

Kamanda wa Jeshi la Polisi Mkoa wa Pwani Wankyo Nyigesa, amewaambia Waandishi wa Habari leo Jumatatu Mei 10, kuwa tukio hilo lilitokea Mei 8, saa 12 alfajiri huko Kibaha kwa Mathias.

Nyigesa, aliwataja wafungwa hao wawili kuwa ni Ramadhani Mohamed 28 (maarufu Seven) Mndengereko mkazi wa kwa Mathias na Idd Hamis(30)Mzaramo mkazi wa Jamaika Kibaha.

Amefafanua kuwa, siku chache baada ya wafungwa hao kusamehewa na Rais kutoka kifungoni  katika gereza la Mkuza Kibaha waliendeleza tabia ya wizi katika katika maduka na maeneo mbalimbali lakini waliingia mikononi mwa wananchi na hivyo kupata kipigo.

Amesema kuwa,watu hao baada ya kukamatwa na wananchi hao walipigwa kwa kutumia silaha za Jadi, Mawe,Mapanga na fimbo waliumia vibaya lakini hatahivyo walifia njiani wakati wakiwa wanakimbizwa hospitali kwa ajili ya kupata matibabu.

“Watuhumiwa walifungwa kwa makosa ya wizi kupitia kesi ya jinai namba 273/2020 na 260/2020 na walipata msamaha wa Rais April 12 mwaka huu katika gereza la Mkuza lililopo Kibaha Mjini lakini baada ya kutoka wakaendelea na tabia yao ya wizi na hivyo kukutana na wananchi na hatimaye kupoteza maisha,”amesema Nyigesa.

Aidha, kutokana na tukio hilo kamanda Nyigesa ametoa rai kwa wananchi kuacha kuchukua sheria mkononi na badala yake wawaachie vyombo vya dola kwa ajili ya kuchukua hatua za kisheria.

Katika hatua nyingine Jeshi hilo limefanya operesheni katika kipindi cha wiki moja katika Wilaya tano za Kipolisi na kufanikiwa kukamata watuhumiwa 21 wakiwemo wanawake watatu.

Kamanda Nyigesa, amesema watu hao wamekamatwa wakiwa na vitu mbalimbali vya wizi walivyoiba katika maeneo tofauti ya Mkoa wa Pwani.

Nyigesa ametaja baadhi ya vitu vilivyokamatwa kuwa ni TV nne aina ya Samsung inch 32,simu za mkononi tatu,kompyuta mpakato mbili aina ya Apple na Dell, Radio aina Kenwood, Pikipiki, Ng’ombe wawili, na vifaa vingine vya umeme.

Hatahivyo, Nyigesa amewaomba wananchi kuendelea kutoa ushirikiano kwa wananchi katika kufichua taarifa mbalimbali za waharifu huku akisema yeyote aliyeibiwa kujitokeza ili haweze kutambua vifaa vyake.

- Advertisement -

Related Articles

LEAVE A REPLY

Please enter your comment!
Please enter your name here

Stay Connected

90,904FansLike
214,997FollowersFollow
586,000SubscribersSubscribe

Latest Articles